Tunakusogezea karibu habari na matukio, zaidi habari za kisiasa na utawala, matukio ya Arusha na maeneo jirani, bila kusahau na mambo mengineyo ya kitaifa yanayojiri katika maeneo mbalimbali ya nchi kuhusu maendeleo na kuwa ya maslahi kwa watu wengi. Burudani na michezo pia havijasahaulika. Kizuri zaidi, unaweza kupata link ya Blogu nyingine na website muhimu hapa hapa kwa kuscroll mpaka chini. Karibu tuhabarike!

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI NA UMMA KUHUSU HATMA YA MSAADA WA FEDHA ZA MCC KWA SERIKALI YA TANZANIA



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI NA UMMA

KUHUSU

HATMA YA MSAADA WA FEDHA ZA MCC KWA SERIKALI YA TANZANIA

Mnamo Desemba 16, mwaka jana, Bodi ya MCC katika kikao chake iliazimia kuahirisha msaada wa USD Mil. 472.8, uliokuwa umekusudiwa kwa ajili ya Tanzania kwa mwaka 2016, ambao ulilenga kusaidia sekta ya nishati ya umeme, hususan maeneo ya vijijini, pia katika kuunganisha wateja wapya na mabadiliko ya kimuundo ya Shirika la Umeme nchini (TANESCO) ili lifanye kazi na kutoa huduma kwa ufanisi katika sehemu za uzalishaji, usafirishaji na usambazaji.

Fedha hizo pia zilikusudiwa kusaidia kuanza kwa mpango mkubwa wa kuboresha sekta ya umeme nchini 2014-2024.

Sababu zilizotumiwa na MCC kuahirisha msaada huo zilikuwa ni pamoja na;

1. Mkwamo wa Uchaguzi wa Rais na Wawakilishi Zanzibar na

2. Matumizi mabaya ya Sheria ya Makosa ya Mtandao hususan

kuhusiana na uchaguzi Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

wa 2015.

Taarifa zilizopo ni kwamba Bodi ya MCC inakutana tena Machi 28, mwaka huu, ambapo pamoja na masuala mengine pia itajadili mchakato wa msaada kwa Serikali ya Tanzania.

Bodi hiyo ya MCC inakutana katika wakati ambapo hakuna hatua zozote za maana zimechukuliwa na Serikali ya Tanzania kurekebisha sababu zile mbili ambazo ziliisukuma bodi hiyo kuahirisha msaada ule mwaka jana.

Sheria ya Makosa ya Mtandao na nyingine zinazofanana na hizo zinazolenga kufifisha uhuru wa habari na kupashana taarifa bado ziko vile vile na hivi karibuni zimetumika hata kufuta kabisa Gazeti la Mawio na kutisha vyombo vingine vya habari pamoja na wanahabari wanaotekeleza wajibu wao kwa jamii.

Hali ya mgogoro wa kisiasa wa Zanzibar imezidi kuwa tete zaidi baada ya Serikali ya CCM kukanyaga demokrasia na kulazimisha kurudia uchaguzi bila msingi wowote unaotokana na uhalali wa kisheria au kisiasa wa kufanya hivyo.

Hivyo basi, wakati Bodi hiyo inakutana kuamua masuala kadhaa ikiwa pamoja na kuhusu hatma ya msaada huo kwa Tanzania, tunapenda kusema yafuatayo katika hatua ya sasa;

Kwa kuwa hadi sasa Serikali haijaonesha nia yoyote ya kupeleka bungeni marekebisho ya sheria mbovu zilizotungwa kwa makusudi kuua uhuru wa habari na maoni/mawazo mabadala, ikiwemo ile ya Makosa ya Mtandao.

Kwa kuwa Serikali badala ya kuziondoa sheria hizo mbovu, imezidi kuzitumia kutisha watu, wakiwemo waandishi wa habari, vyombo vya habari ina sasa imekwenda hatua kubwa zaidi hata ya KUFUTA chombo cha habari (Gazeti la Mawio).

Kwa kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano chini ya Rais Magufuli imeamua kupuuza kabisa maoni ya Watanzania waliotaka imalize mgogoro wa kisiasa nchini Zanzibar kwa kumtangaza mshindi halali aliyepatikana katika uchaguzi mkuu Oktoba mwaka jana.

Kwa kuwa Serikali ya Tanzania, kinyume kabisa na misingi ya uhalali wa kisheria na kisiasa imeamua kusigina demokrasia huko Visiwani na kulazimisha kurudia uchaguzi ambao tayari ulishafanyika.

Kwa sababu Serikali ya Tanzania haijatambua umuhimu wa sheria zinazotenda haki, kuzingatia demokrasia na utawala bora kuwa ni misingi imara ya amani na utulivu wa kweli, maendeleo chanya na ustawi wa jamii;

Tunaamini kuwa Bodi ya MCC itaungana na Ubalozi wa Marekani pamoja na Mabalozi wa Nchi za Jumuiya ya Ulaya nchini Tanzania, Kulaani kilichofanyika Zanzibar.

Kuendelea kutoa wito kwa Serikali kufuta au kuzifanyia marekebisho sheria zinazolenga kuua uhuru wa habari na maoni kwa ujumla.

Kuitikia wito wa kuendelea kuahirisha mchakato wa msaada huo kwa Serikali ya Tanzania hadi hapo Serikali hii itakapoona umuhimu wa kuwa na mwafaka wa kitaifa kuamua hatma ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ujumla wake, yenye amani na utulivu unaosimama katika misingi ya demokrasia na uongozi bora unaozingatia sheria zinazotenda haki.

Pamoja na mambo mengine, bodi hiyo izingatie na kujiridisha iwapo Serikali ya Tanzania imeamua kutambua umuhimu wa misingi hiyo katika kuondoa chembechembe za udikteta zinazoanza kuonekana kutoka kwa utawala wa awamu ya tano.

Itakumbukwa kuwa Bodi ya MCC ilipoamua kuahirisha mchakato wa kuipatia fedha Serikali ya Tanzania, mwaka jana, CHADEMA tulitoa kauli kuwa kuchelewa kupatikana kwa fedha za MCC si tu kunachafua jina la nchi na hadhi yake katika medani za kimataifa, bali kutaathiri kwa kiasi kikubwa miradi yote iliyo chini ya ufadhili wa MCC.

Kuhusu Sheria ya Makosa ya Mtandao 


Tulisema pia kuwa Sheria ya makosa ya mtandao (Cyber Crime Act 2015) ni sheria mbaya sana inayokinzana na kukua kwa technolojia ya habari na mawasiliano ambapo watawala chini ya utawala wa CCM, walilenga kwa makusudi kuua uhuru wa kupeana taarifa na kupashana habari.

Kumbukumbu zinaonesha kuwa sheria hiyo ilipitishwa usiku wa manane kwa ubabe wa wabunge wa CCM na hata tulipomtaka Rais Jakaya Kikwete kwa maslahi mapana ya taifa asiisaini, aliisaini kibabe akijua anaandaa mazingira gani ya ‘kihalifu’ dhidi ya uhuru wa kutafuta, kupokea na kusambaza taarifa, wakilenga kudhibiti kijinai uchaguzi mkuu uliopita.

Sheria hiyo ilitumika kuhalalisha ‘uvamizi’ wa vituo vya CHADEMA vilivyokuwa vikitumika kukusanya matokeo ya kura za rais na wabunge na hadi leo vijana zaidi ya 161, wakiwemo wanafunzi, wana kesi za “kubumba” mahakamani, huku CCM wakiwa na vituo vilivyokuwa vikifanya kazi hiyo hiyo na Jeshi la Polisi halikudhubutu kuvizuia achilia mbali kuwakamata waliokuwemo na kuwafungulia kesi.

Ni sheria hiyo hiyo ilitumika kuficha dhana ovu iliyotumika kuhalalisha kuvamia Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kilichokuwa kikiratibu watazamaji wa uchaguzi wa ndani kwa kibali cha Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).

Tulitoa rai kwa Rais John magufuli kuchukua hatua za kiuongozi kuifanyia marekebisho makubwa Sheria ya Makosa ya Mtandao kupitia bungeni, pia kumuagiza DPP kuzifuta kesi ambazo watu wamebambikiwa kutokana na sheria hiyo mbovu.

Kuhusu Zanzibar

Tulimtaka Rais Magufuli aingilie kati na kumaliza mgogoro wa kisiasa uliokuwa unaiweka Zanzibar katika hali tete ambapo wito wetu ulisisitiza kuhakikisha kuwa mshindi halali aliyepatikana katika uchaguzi mkuu mwaka jana natangazwa badala ya kuiacha nchi katika sintofahamu na kulazimisha uchaguzi wa marudio bila kuwepo na uhalali wowote wa kisheria wala kisiasa kufanya hivyo.

Imetolewa leo Jumatatu, Machi 28, 2016 na;

Idara ya Habari na Mawasiliano

CHADEMA
Washirikishe Google Plus

About Unknown

SeriaJr will keep you updated with all current political news countrywide "Ndiye "Bosi" Mzito Arusha255" Karibu Tuhabarike!.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 maoni:

TANZANIA, THE HOME OF KILIMANJARO