Tunakusogezea karibu habari na matukio, zaidi habari za kisiasa na utawala, matukio ya Arusha na maeneo jirani, bila kusahau na mambo mengineyo ya kitaifa yanayojiri katika maeneo mbalimbali ya nchi kuhusu maendeleo na kuwa ya maslahi kwa watu wengi. Burudani na michezo pia havijasahaulika. Kizuri zaidi, unaweza kupata link ya Blogu nyingine na website muhimu hapa hapa kwa kuscroll mpaka chini. Karibu tuhabarike!

JAJI: MAHAKAMA ILIINGILIWA VIBAYA KESI YA LEMA

Imeandika wa JANETH MUSHI Na ELIYA MBONEA-ARUSHA

VILIO, shangwe na nderemo jana vilitawala katika Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, baada ya Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema (Chadema), kuachiwa huru kwa dhamana.

Mwanasiasa huyo machachari ameachiwa huku akiandika rekodi ya kukaa mahabusu katika Gereza Kuu la Kisongo kwa zaidi ya miezi minne baada ya kukosa dhamana.

Lema aliachiwa kwa dhamana jana wakati mahakama hiyo ilipokuwa ikisikiliza rufaa ya Jamhuri namba 135 ya mwaka jana, inayopinga uamuzi wa Novemba 11, mwaka jana wa Hakimu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, Desderi Kamugisha wa kumpa Lema haki ya dhamana.

Shangwe zililipuka katika ukumbi huo wa mahakama mara baada ya Jaji Salma Maghimbi wa mahakama hiyo kumwachia Lema kwa masharti ya kujidhamini mwenyewe pamoja na kudhaminiwa na wadhamini wengine wawili ambao kila mmoja alisaini hati yenye thamani ya Sh milioni moja.

Akitoa uamuzi huo, Jaji Maghimbi alisema mahakama ya chini ilishindwa kusimamia mamlaka yake vizuri hivyo kuingiliwa kabla haijamaliza mwenendo wake.

Jaji huyo alisema mahakama ikitamka dhamana iko wazi inatakiwa kukamilisha zoezi hilo ikiwa ni pamoja na mshtakiwa kudhaminiwa na kama upande wa pili utakata rufaa kupinga ufanye hivyo  baada ya uamuzi kutolewa.

Pamoja na hilo alisema kwa mamlaka iliyonayo Mahakama Kuu ya kuzisimamia mahakama za chini baada ya kubaini tatizo kuanzia mazingira ya kesi hiyo na Lema kukaa gerezani muda mrefu, iliamua kujivika madaraka ya kukamilisha masharti ya dhamana yenyewe.

Jaji Maghimbi alisema Mahakama Kuu imeamua kumalizia kazi iliyopaswa kufanywa na mahakama ya chini na hivyo kutangaza kufuta notisi ya kusudio la kukata rufaa iliyotolewa na mawakili hao Novemba 11, mwaka jana kwa kile alichosema ilikosa mashiko na misingi ya kisheria.

“Nashangaa hakimu aliruhusu vipi mtu asimame wakati wa mwenendo, hivyo nakubaliana na hoja za wajibu rufaa na mahakama ilipaswa kusubiri mpaka mwisho ikague wadhamini na ninakemea mahakama za chini zisimamie madaraka yake kwa sababu isiposimamia madaraka yake vizuri itachezewa na watu hawatapata haki zao,” alisema Jaji huyo.

Katika rufaa hiyo mawakili wa Serikali walikuwa wakipinga mahakama ya chini kumpa Lema dhamana kwa vielelezo kuwa usalama wa mwanasiasa huyo utakuwa hatarini iwapo atakuwa nje.

Lema alikuwa akiwakilishwa na jopo la mawakili wanne wakiongozwa na Peter Kibatala, Adam Jabir, Sheck Mfinanga na Faraji Mangula wakati Jamhuri iliwakilishwa na Faraja Nchimbi na Paul Kadushi.

RUFAA YA LEMA YAONDOLEWA

Baada ya uamuzi huo, mawakili wa Lema waliomba kuondoa mahakamani hapo rufaa namba 126 iliyokatwa na mbunge huyo dhidi ya Jamhuri ambayo ilikuwa inapinga na kudai haki ya dhamana ya kiongozi huyo.

Baada ya rufaa ya Jamhuri kufutwa, huku akilia wakili Kibatala naye aliiomba mahakama hiyo kufuta rufaa ya mteja wake kutokana na kupewa dhamana, ambapo jaji alikubali ombi hilo.

ILIVYOKUWA MAHAKAMA ZA CHINI

Novemba 11, mwaka jana, Wakili Mwandamizi wa Serikali, Paul Kadushi, alisimama wakati hakimu huyo akijiandaa kuandika masharti ya dhamana na kuieleza mahakama hiyo kuwa wameshasajili notisi ya kusudio la kukata rufaa Mahakama Kuu wakipinga uamuzi wa hakimu huyo kumpa Lema dhamana.

Hata hivyo, uamuzi huo wa dhamana haukuweza kutekelezwa kwa sababu ya nia ya kukata rufaa waliyoitoa mawakili hao wa Serikali.

Hakimu Kamugisha alishindwa kuendelea na masharti ya dhamana kwa mshtakiwa huyo ambapo alikubaliana na upande wa Jamhuri na kusema kuwa notisi ina hadhi sawa na maombi ya rufaa yaliyowasilishwa Mahakama Kuu hivyo mwenendo na uamuzi wake utasimama hadi uamuzi utakapotolewa na Mahakama Kuu.

Januari 4, mwaka huu, Jaji Maghimbi alitarajiwa kusikiliza na kutoa uamuzi kuhusiana na dhamana ya Lema hata hivyo ilikwama baada ya mawakili wa Serikali kukata rufaa Mahakama ya Rufaa Tanzania, kupinga Jaji huyo  kusikiliza rufaa yao wenyewe.

CHANZO:

Washirikishe Google Plus

About Unknown

SeriaJr will keep you updated with all current political news countrywide "Ndiye "Bosi" Mzito Arusha255" Karibu Tuhabarike!.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 maoni:

TANZANIA, THE HOME OF KILIMANJARO