TIMUN huandaliwa na Shirikisho la vijana wa Umoja wa Mataifa (YUNA) taasisi ya vijana isiyotengeneza faida inayotangaza shughuli za Umoja wa Mataifa na kushirikisha vijana katika utekelezaji wa shughuli hizo. Aidha aliwashukuru waandazi wa mkutano huo kubwa unaofanana na Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa (General Assembly) wenye lengo la kukutanisha vijana kujadili mustakabali wa malengo ya dunia. Alisema vijana wana nafasi muhimu katika utekelezaji wa malengo hayo ya maendeleo endelevu jukumu ambalo dunia imejipa kwa miaka 15 hadi mwaka 2030. Pamoja na kuwashukuru Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, Arusha (NM-AIST) kwa kukubali kuwa mwenyeji wa kambi hiyo, hali iliyoonesha kwamba wanajali vijana, mwakilishi huyo wa serikali alisema kwamba Tanzania ipo tayari kusukuma mbele ajenda ya ushirikishaji vijana katika maendeleo endelevu kwa kuwa inaamini juu ya hilo.
Alisema kwamba malengo ya dunia ambayo yapo 17 yanagusa kila sehemu ya maisha na hivyo ni vyema kama vijana watatoka na majibu ya maswali yanaoumiza vichwa kuhusu malengo hayo hasa mazingira na dunia endelevu. Aliwataka vijana kutumia nafasi yao vyema katika jukwaa hilo kwani maisha ya watu bilioni 7 duniani wanategemea namna ambavyo wanajengwa na vijana, wenye mchango muhimu wa kulinda mazingira na kuhakikisha maendeleo endelevu.
Awali Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez alisema kwamba zaidi ya vijana elfu 20 nchini Tanzania wamefunzwa malengo endelevu ya dunia, toka ulipofanyika uzinduzi Juni, 2016. Akizungumza katika hafla ya kambi ya mwaka huu ya Tanzania International Model United Nations (TIMUN), inayofanyika katika Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, Arusha (NM-AIST), Bw. Rodriguez alielezea kufurahishwa na idadi hiyo ya vijana waliohamasishwa na kusema kwamba malengo ya maendeleo endelevu 2030 yanahitaji kila mmoja kushiriki. Aidha alielezea umuhimu wa ushiriki wa vijana katika masuala ya maendeleo kutokana na uwingi wao hapa nchini. Asilimia 67 ya watu nchini ni vijana.
Bw. Rodriguez alishukuru machampioni kwa kuwezesha vijana wenzao kutambua malengo endelevu ya dunia na kuwataka kuendelea kufanya vizuri zaidi katika kuwashawishi vijana wenzao kuelewa na kushiriki katika malengo hayo. “Nataka kuwatafadhalisha kwamba huu ni mwanzo tu, kuna mengi ya kufanya. Kama Umoja wa Mataifa, tunawataka wote mshiriki, si tu katika kuelimisha kuhusu malengo haya ya dunia, lakini pia katika kuangalia mwenendo wa maendeleo hayo katika jamii na namna yanavyotekelezwa. Tukio kama hili la TIMUN linasaidia kuongeza uwezo wa kufikia malengo ya dunia,” alisema Bw. Rodriguez. Vijana 50 wa kwanza machampioni walifunzwa mwaka jana katika TIMUN 2016. Kwa sasa kuna vijana machampioni 500 nchini Tanzania ambao wamepeleka ujumbe kwa vijana wenzao 20,000.
Ujumbe ambao umekuwa ukisambazwa na machampioni kwa wenzao umeelezwa kulenga kuchochea hamasa ya kuelewa malengo kwa ajili ya maendeleo. “Kama watu hawatajua malengo ya maendeleo endelevu, hawataweza kufanya malengo hayo kuwa ya kweli,” aliusema ujumbe huo Gloria Nassary, ambaye ni mmoja kati ya vijana 50 waliopewa mafunzo ya kwanza ya kuwa machampioni wa malengo ya dunia. Naye Tajiel Urioh ambaye ni Mratibu wa Mkutano Mkuu wa Kimataifa wa Baraza Kivuli la Vijana la Umoja wa Mataifa (TIMUN 2017), pamoja na kusisitiza amani kama sehemu muhimu ya kusukuma mbele utekelezaji wa malengo 17 ya maendeleo endelevu aliwahimiza vijana kutokata tamaa katika kuhimiza utekelezaji wa malengo hayo.
Alisema bila amani kuanzia katika ngazi ya familia, uwezekano wa kutekeleza malengo hayo unakuwa mgumu kwa kuwa kuna uhusiano mkubwa kati ya amani na utekelezaji wake. Alisema amani ni kionjo muhimu cha maendeleo kinapokosekana hata jukumu la vijana kulinda mazingira kwa ajili ya maendeleo endelevu halitawezekana. Alisisitiza kulinda mazingira kwa ajili ya maendeleo na kufikiwa kwa malengo ya Umoja ya Mataifa ambayo ni malengo ya dunia katika kuimarisha ustawi wa jamii na kuinua uchumi . Urioh katika mazungumzo yake alisema suala la uchafuzi wa mazingira ni suala gumu na mtambuka na kwamba mabadiliko ya tabia nchi yanayosababishwa na kuvurugwa kwa tabaka la ozoni halihusu Ulaya pekee, ambao wanachafua bali kila mmoja duniani; akiongeza kuwa mwishoni mwa siku wanaoathirika ni zaidi nchi zinazondelea akitolea mfano nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara.
Alisema suala la kukabilina na mabadiliko ya tabia nchi si kutulia bali kuwajibika kutekeleza wajibu ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba hakuna uharibifu wa mazingira unaofanyika katika taifa la Tanzania. Alisema vijana wanaweza kufanya zaidi ya yale ambayo kwa sasa wameyafanya katika kutekeleza malengo ya maendeleo endelevu kwa kuhakikisha kwamba wana elimu ya kutosha kuhusu malengo hayo na kushirikiana kuyatekeleza kwa kuangalia changamoto mbalimbali ambazo wanazipatia majibu. Alisema lengo la malengo hayo ni kusaidia jamii vivyo hivyo vijana nao wanatakiwa kujitoa mhanga kuhakikisha kwamba jamii inaendelea kustawi na kuendelea kwa manufaa ya kizazi kijacho.
Aliwataka vijana kutafuta majawabu ya mambo yanayoikabili dunia kwa namna ya busara na kitaalamu zaidi huku wakizingatia diplomasia. Septemba 2015, wanachama 193 wa Umoja wa Mataifa walikubaliana juu ya malengo mapya ya dunia, malengo ya maendeleo endelevu. Malengo hayo yanatarajiwa kufanyiwa kazi katika kipindi cha miaka 15 ijayo na kuleta mabadiliko makubwa katika jamii, uchumi na mazingira kwa namna ya kuwa endelevu.
Wakati akiwa Arusha, Mratibu pia alifuatilia matokeo ya mafunzo yaliyofanyika Novemba mwaka jana katika chuo kikuu cha Tumaini Makumira yaliyofanywa kwa pamoja kati ya Umoja wa mataifa na Jumuiya ya Ulaya. Katika mafunzo hayo machampioni 80 walifunzwa wakiwemo wanachuo 30 kutoka Taasisi ya Uhasibu ya Arusha (Institute of Accountancy Arusha -IAA). Mkutano huo umefadhiliwa Umoja wa Mataifa (UN), Serikali, Covenant Bank, Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, Arusha (NM-AIST) pamoja PIU.
KAWAIDA Vijana kutoka mataifa mbalimbali waliokusanyika katika Mkutano Mkuu wa Kimataifa wa Baraza Kivuli la Vijana la Umoja wa Mataifa (TIMUN), mjini Arusha wametakiwa kuchambua masuala yaliyopo mbele yao kwa makini ili kutoa jawabu kwa matatizo ya dunia yanayohitaji ushiriki wao. Kauli hiyo imetolewa na mwakilishi wa serikali katika mkutano huo Ngusekela Karen Nyerere, Ofisa anayeshughulikia dawati la Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Aliwataka vijana wanaoshiriki TIMUN kuhakikisha wanaangalia kwa makini mambo yanayogusa nchi zao na kuyatafutia ufumbuzi kwa kuwa ndio njia pekee ya kutekeleza malengo endelevu ya dunia ambayo yanahitaji ushirikiano wa ndani na wa kimataifa. TIMUN ambayo kirefu chake ni Tanzania International Model United Nations hufanyika kila mwaka na ujumbe mbalimbali na mwaka huu ujumbe wa TIMUN ni: “kuwawezesha vijana katika diplomasia na uongozi”
0 maoni:
Post a Comment