Tunakusogezea karibu habari na matukio, zaidi habari za kisiasa na utawala, matukio ya Arusha na maeneo jirani, bila kusahau na mambo mengineyo ya kitaifa yanayojiri katika maeneo mbalimbali ya nchi kuhusu maendeleo na kuwa ya maslahi kwa watu wengi. Burudani na michezo pia havijasahaulika. Kizuri zaidi, unaweza kupata link ya Blogu nyingine na website muhimu hapa hapa kwa kuscroll mpaka chini. Karibu tuhabarike!

Pengo asema Shule TZ zimekuwa vitega uchumi

ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amesema elimu inayotolewa nchini ni ya kibaguzi.

Kardinali Pengo alisema hayo Dar es Salaam jana alipokuwa akiwasilisha ujumbe wa maaskofu wa Kanisa Katoliki walioutoa katika mkutano wao uliofanyika Oktoba 7 hadi 28, mwaka huu huko Roma, Italia.

Alisema watu wote wenye mapenzi mema na nchi hii wanapaswa kutoa kipaumbele katika upatikanaji wa elimu bora kwa kila Mtanzania.

Kardinali Pengo alisema hapendezwi na namna elimu inavyotolewa nchini kwani kimfumo, baadhi ya shule zimekuwa vitegauchumi, hivyo kuwa kikwazo kwa watu wenye kipato cha chini.

“Wenye vipato vya chini hawawezi kusoma katika shule hizi kwa sababu zinatoza ada kubwa ambayo maskini hawezi kumudu gharama zake,” alisema.

Askofu Pengo alionya kuwa endapo hali hiyo itaachiwa, inaweza kuwafanya wale waliokosa elimu kuwa chanzo cha vurugu kwa kuwa watasimama kidete kudai haki yao.

Maoni ya Katiba
Katika hatua nyingine, Kardinali Pengo alizungumzia mchakato wa Maoni ya Katiba unaoendelea nchini, huku akiwaonya baadhi ya wanasiasa na taasisi mbalimbali za dini kuacha kuwashinikiza wananchi kutoa maoni kwa ajili ya masilahi yao binafsi.

“Kila mtu aruhusiwe kutoa maoni yake, lakini lazima tukubaliane kuwa kila mtu ana maoni yake na maoni yote hayawezi kuingizwa katika Katiba Mpya,” alisema Pengo.

Alisema kwa kuwa Katiba inagusa masilahi ya nchi, ni vyema kila mwananchi akatumia fursa yake ya kuwasilisha maoni yake mwenyewe.

Alitahadharisha kuwa wananchi wasiposhirikishwa katika mchakato wa Katiba Mpya, wanaweza kuja kuikataa kwa sababu maoni yao hayakuzingatiwa.

Suala la udini
Kiongozi huyo wa Kanisa Katoliki  wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, ameitaka Serikali kuchukua hatua za makusudi kwa wale wote watakaobainika kusababisha uharibifu wa mali za dhehebu la dini yoyote hapa nchini, kama wanavyofanya pindi kunapotokea uhalifu katika benki au wizi katika maeneo ya viongozi na sehemu nyingine.

Alisema nchi imegawanyika katika madhehebu mbalimbali, hivyo inapotokea dhehebu moja kulitukana na kuharibu mali za jingine, Serikali haipaswi kukaa kimya.

Alisema Serikali inapaswa kuwa makini, ikiwamo kuwafuatilia na kuwachukulia hatua wale wote wanaoonyesha dalili za uvunjifu wa amani.

Aliwataka viongozi wenye dhamana kuacha kushabikia udini katika kusimamia haki za jamii kwa Watanzania.

Kardinali Pengo pia aliitaka Serikali kuchukua hatua juu ya mihadhara isiyofaa majukwaani.

“Mungu ametuumba ili tumwabudu kila mtu kwa dini yake, huna sababu ya kumtukana mwenzako au kuikashifu dini ya mwenzako, tunachotakiwa ni kufuata misingi na mema yote,” alisema.

Alisema kama Serikali inashindwa kuwakemea na kuwachukulia hatua wale wanaowatukana wenzao, hali hiyo ikiachwa inaweza kuvuruga amani na mshikamano na hivyo nchi kuingia kwenye mgogoro wa kidini.

Kardinali Pengo alisema haoni tatizo kama mtu atasema Yesu si mwana wa Mungu katika nia na mtazamo wake na mwingine akasema Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu na siyo kutupiana maneno ambayo mwisho wa siku inakuwa ni chuki kubwa.

Chanzo: Mwananchi 14/12/2012

Washirikishe Google Plus

About SeriaJr

SeriaJr will keep you updated with all current political news countrywide "Ndiye "Bosi" Mzito Arusha255" Karibu Tuhabarike!.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 maoni:

TANZANIA, THE HOME OF KILIMANJARO