Tunakusogezea karibu habari na matukio, zaidi habari za kisiasa na utawala, matukio ya Arusha na maeneo jirani, bila kusahau na mambo mengineyo ya kitaifa yanayojiri katika maeneo mbalimbali ya nchi kuhusu maendeleo na kuwa ya maslahi kwa watu wengi. Burudani na michezo pia havijasahaulika. Kizuri zaidi, unaweza kupata link ya Blogu nyingine na website muhimu hapa hapa kwa kuscroll mpaka chini. Karibu tuhabarike!

SERIKALI KANDAMIZI HUSABABISHA UASI NDANI YA NCHI - Waraka wa Godbless Lema


lema arusha 10 decNimetazama habari za vyombo za habari leo asubuhi na kutafakari nafikiri napaswa kuweka kumbukumbu vyema na sahihi bila kumumunya maneno hata kidogo.
Nimekuwa Bunda na Musoma katika ujenzi wa Chama na jana tarehe 10/12/2012 nilifanya mkutano Arusha Mjini wenye ujumbe unaofanana na nilioutoa Bunda na Musoma na ambao nitaupeleka Nchi nzima kuanzia January bila kupumzika wala kuchoka mimi na makamanda wengine ambao sasa tumeamua ni “ DIE or LIVE .
Nimeamua kusema na nitaendelea kusema popote nitakupokuwa kuwa “ Ni afadhali vita inayotafuta haki na usawa kuliko amani inayopumbaza na kudhalilisha utu wa Mwanadamu , nilipokuwa Musoma na Bunda niliwaambia Wananchi hao kuwa wakati wakuendelea sisi Watanzania kuwa wajinga umekwisha na lazima tuhufikishe mwisho.
Maisha yameendelea kuwa Magumu sana kila siku , hakuna haki wa usawa katika mambo muhimu ya maisha , wezi wakubwa wanaohujumu pesa za umma wanaendelea kuwa na neema kubwa na ya kupindukia huku watu katika Taifa hili wanaendelea kuwa Masikini wakupindukia na kuishi maisha ya aibu kubwa katika jamii huku dada zetu wakiishia kuuza miili yao na marafiki zetu wakiishia jela kwa udokozi unaotafuta kushinda njaa zao tu za kila siku.
Ni mpaka lini tutaendelea kukaa kimya tunaposikia wezi na wabadhirifu wa mali ya Umma wameibia na kuipotezea Taifa bilioni elfu tisa ( 9000,000,000,000) wakipewa adhabu ya kujiuzulu uwaziri na huku mwizi wa simu Manzese anafungwa miaka kumi jela ? huko wapi usawa na Amani katika Taifa hili ?
Hivi karibuni tumesikia kutoka Bungeni pesa nyingine nyingi zimefichwa huko New Jersey , Dubai , Uswisi na kwingine kwingi na haya ni mabilioni ya Walipa kodi wa Watanzania na Wabunge wanasema wawajua lakini hawawezi kuwataja , hiki ni kichekesho kwani kutaja mwizi na kwenyewe kunataka itifaki ? na sisi tunapata huzuni eti wanaposwa kusimamia sheria na utawala wa Serikali wanahitaji itifaki kuwataja Majambazi na Majangili wanaoendelea kuangamiza maisha ya Nchi yetu na mimi niombe Nipewe hayo majina ninajua kwa sasa sina kinga ya Bunge lakini nitawataja bila kumuogopa Mtu yeyote wa cheo chochote.
Ushauri wangu kwa wabunge wa vyama vyote sio kila jambo unahitaji mwongozo wa Spika wakati mwingine unahitaji mwongozo wa haki na ukweli hata kama Spika hataki , hatuwezi kusema eti Spika hakunipa nafasi ikawa ni sababu ya kuficha majambazi na majangili wa pesa zetu , kuvunja utaratibu au sheria kwa kupigania haki na ukweli ni jambo linalokubalika Mbinguni na Duniani , kama Mwl Nyerere , ,Nelson Mandela na Martin Luther Jr walipovunja sheria za wakandamizaji ili kupigania uhuru wa msingi na haki za watu wao.
CCM na Serikali yake Dhaifu wamekuwa wakifanya mzaha na amani ya Nchi yetu kwa kuendelea kupuuza utawala bora katika Taifa letu , dharau wanayoonyesha kwa Watanzania ni kubwa sana , na msaada wao katika kutekeleza mambo machafu ya ufisadi unatokana na namana walivyoweza kuthibiti vyombo vya usalama, sasa swali je tutaendelea kuona Nchi inaporwa na kuishia eti kwa sababu CCM na serikali yake wanaongoza polisi na Majeshi ? Mimi siwezi kuishi nyakati hizi nikitazama mambo haya Nelsom Mandela alisema “Serikali au utawala unapotumia mabavu kumkandamiza mtu mnyonge kimsingi haimfundishi mtu huyo kuwa dhaifu bali humfundisha mtu huyo kutafuta njia za kujitetea dhidi ya uonevu “
Nchi yetu ilipoingia vitani na Uganda mwaka 1978 , Nyerere alisema “ tunakwenda kumpiga Idd Amin , kwani Sababu tunazo , Nia Tunayo na Uwezo tunao .
Sababu ya vita ilikuwa ni kupinga uvamizi wa Nduli Idd Amin na nia ilikuwa ni kutetea dhamira njema na masilahi ya wananchi ,rasilimali na mipaka ya Nchi yetu hivyo basi hata kama hatukuwa na uwezo ilitupasa kutafuta uwezo ili kutetea Nchi yetu na watu wetu.
Kuna uchaguzi mwaka 2015 na haya nimesema Musoma na sasa naandika kama kumbukumbu muhimu ambayo niko radhi kwenda nayo popote hata kunyongwa, Watanzania watachagua Rais , Wabunge na Madiwani tunataka uchaguzi huru na wa haki Chadema au Chama chochote cha siasa kikishinda kwa haki kitangazwe mara moja kuwa mshindi , lakini jaribio lolote lakutaka kupindisha haki katika uchaguzi linaleta moja kwa moja tafsiri kuwa uchaguzi wa kura hauwezi kuleta mfumo mpya wa utawala Tanzania na mimi ndipo najiuliza sasa unataka tukiibiwa kura kwa nguvu sisi tufanyeje ? twende Bar tukacheze Darts ? Mabadiliko katika Taifa letu sio ombi ni lazima na kama tutakuwa na sababu , na nia , basi uwezo wa kupigania uhuru wa pili kati Taifa letu kwanini tusitafute ? Maisha ya Watanzania lazima yabadilike ,. Rasilimali lazima zitumike kwa manufaa ya wote na sio viongozi na familia zao ,naniliposema Tanzania isipokuwa makini watazaliwa M23 wengine kwani siku zote vikundi vya waasi vinazaliwa na Serikali na utawala Kandamizi.
January Makamba alisema “ Upinzani kamwe usitarajie kamwe kuwa kuna siku watapewa Nchi hii kuongoza “ Na mimi ni mjibu hii Nchi sio ya baba yake , hii Nchi ni mali ya Watanzania wote na yeyote atakayeshinda uchaguzi kwa haki na kweli ataongoza Nchi na wakifikiri wanaweza kupora ushindi kwa nguvu basi watu wema pia watakuwa na sababu na nia ya kutafuta haki ambayo kimsingi huwa aiombwi .
Ni lazima sana tunapoelekea kwenye uchaguzi Mkuu watawala wajue vita na ghasia mara zote zinasababishwa na mfumo mbaya wa utawala na kwa hali ya maisha ilivyo kinachoifanya Tanzania kuwa na utulivu sio sera nzuri za CCM kama Chama Tawala bali ni uungwana wa Watanzania ambao na hakika wamekaribia kuchoka na ni hatari kubwa mtu mpole akichoka na kusema sasa basi.
Kwa hiyo katika kipindi hiki tunachoangahika kutafuta usawa katika mambo ya msingi katika jamii , Maneno yetu kwa Watanzania ni kuwafundisha ujasiri na utiyari wa kuokoa Nchi yao ambayo imekwishateketezwa na kikundi cha wahuni wachache ambao hawaoni Aibu kuiba wala kuua kila siku . Tukatae kwa nguvu zote kuburuzwa . kuonewa , na Taifa letu kuibiwa kila kitu na ukitazama Sekretarieti Mpya ya CCM utaona mafisadi wa zamani wenye uzoefu tofauti wa wizi wamerudi tena katika madaraka ya Chama Tawala
Kila mtu anawajibu wa kukekemea uozo katika Taifa letu na kupinga vikali kikundi cha uasi kilichoko Tanzania kinachoitwa CCM kwani kazi yake ni kuiba , kupora , kutaifisha na kuua .
Hivyo basi ujasiri ni kipimo sahihi , tusirudi Nyuma , tusonge mbele kila mtu kwa nafasi yake na uwezo wake katika kunusuru Taifa hili.
Mwisho nimesikia pia propaganda nyingine nyingi kuhusu mimi zimesomwa kwenye magazeti ya kufungia vitumbua , kwa sasa sina muda wa upuuzi huo kwani wakati na ukimya mara nyingi ni nguvu kubwa katika kujibu habari za kidaku na umbeya .
“Ni kheri Mwanadamu akaishi miaka michache duniani jina lake likabaki linaishi kwa haki na wema kuliko miaka mingi na ukatoweka kama mzoga “ STEVEN BIKO
GODBLESS J LEMA

11 Disemba 2012

Washirikishe Google Plus

About SeriaJr

SeriaJr will keep you updated with all current political news countrywide "Ndiye "Bosi" Mzito Arusha255" Karibu Tuhabarike!.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

1 maoni:

Anonymous said...
This comment has been removed by the author.

TANZANIA, THE HOME OF KILIMANJARO