Tunakusogezea karibu habari na matukio, zaidi habari za kisiasa na utawala, matukio ya Arusha na maeneo jirani, bila kusahau na mambo mengineyo ya kitaifa yanayojiri katika maeneo mbalimbali ya nchi kuhusu maendeleo na kuwa ya maslahi kwa watu wengi. Burudani na michezo pia havijasahaulika. Kizuri zaidi, unaweza kupata link ya Blogu nyingine na website muhimu hapa hapa kwa kuscroll mpaka chini. Karibu tuhabarike!

CHADEMA yataka Zitto achunguzwe

na Edson Kamukara, Dodoma

zitto KAMBI rasmi ya Upinzani Bungeni imetaka kuchunguzwa kwa madai ya Naibu Kiongozi wa wa kambi hiyo, Zitto Kabwe, kuhongwa.

Kambi hiyo pia imetaja majina ya wabunge sita wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), waliokuwa wajumbe wa Kamati ya Nishati na Madini iliyovunjwa na Spika wa Bunge, Anne Makinda, mwishoni mwa wiki, ikidai kuwa kwa namna moja ama nyingine walihusika na vitendo vya rushwa.

Wabunge hao wanatuhumiwa kupokea rushwa kutoka kwa kampuni za mafuta ili kuipigia debe menejimenti ya Shirika la Ugavi wa umeme nchini (TANESCO).

Akizungumza jana na waandishi wa habari mjini hapa, Mnadhimu Mkuu wa kambi hiyo, Tundu Lissu, alisema wamesikia tuhuma nyingi dhidi ya Zitto lakini hawajamhoji kiongozi huyo.

Alisema wanaviomba vyombo vinavyohusika vimchunguze Zitto ili ukweli ujulikane na hatua zinazostahili zichukuliwe kama atathibitika kuwa na makosa.

“Chama hatujakaa na Zitto kumsikiliza lakini tunataka achunguzwe, hatuna masilahi yoyote katika uchafu huu wa rushwa.

“Uchunguzi huu utatupa msingi wa kumchukulia hatua kama chama ikiwa itathibitika amehongwa,” alisema.

Alibainisha kuwa, mbunge wao huyo amekuwa akihusishwa na kumtumia ujumbe mfupi wa vitisho Katibu Mkuu wa Nishati na Madini, Eliakimu Maswi.

Alisema ni vema Zitto achunguzwe na apewe nafasi ya kujieleza kama itakavyokuwa kwa wengine kuliko kuendelea kusambaza maneno ya kufikirika.

Alibainisha wamejiridhisha pasipo shaka kuwa wabunge wao watatu waliokuwa wajumbe kwenye Kamati ya Nishati na Madini, John Mnyika (Ubungo), David Silinde (Mbozi Magharibi) na Mwanamrisho Taratibu Abama (Viti Maalumu), hawajahusika kwa lolote katika sakata hilo la rushwa.

“Kama kuna mtu ana ushahidi zaidi ya huu tulionao tunaomba atuletee ili hatua zaidi ziweze kuchukuliwa, lakini mpaka sasa wabunge wetu hawa watatu hawajashiriki kwa lolote katika kuomba rushwa,” alisema.

Kauli ya Lissu inashabihiana na aliyoitoa Zitto juzi ambapo alisema hajachukua hongo, ila kuna watu wana lengo la kuchafua jina lake.

Zitto alisema kuwa uchunguzi dhidi yake ndiyo njia pekee ya kuudhihirishia umma kuwa hahusiki na chochote kama baadhi ya watu wanaoeneza maneno ya kumchafua.

Awataja wala rushwa

Kuhusu majina ya wabunge wanaotuhumiwa kujihusisha na vitendo vya rushwa, Lissu alisema kuwa kwa mujibu wa kanuni za kudumu za Bunge na Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma ya mwaka 1995, wabunge hao walipaswa kutaja masilahi yao kibiashara kwenye shirika hilo.

“Sasa wabunge hawa hawajawahi kufanya hivyo na wameendelea kuwa wajumbe wa Kamati ya Nishati na Madini na wengine kufanya biashara na TANESCO,” alisema Lissu na kuwataja kuwa ni Munde Tambwe, Sara Msafiri, Mariam Kisangi wa Viti Maalumu, Yusuf Nassir (Korogwe Mjini) na Charles Mwijage Muleba Kaskazini.

Lissu alifafanua kuwa Tambwe na Msafiri wana tenda ya kuiuzia TANESCO matairi na kwamba hawajawahi kutangaza masilahi yao katika jambo hilo kwenye kamati zao.

“Mwijage ni mtaalamu mwelekezi wa Kampuni ya PUMA Energy iliyopewa tenda na Maswi kuiuzia mafuta TANESCO, hivyo kama mjumbe wa Kamati ya Nishati ana mgongano wa kimasilahi. Nassir na Kisangi hawa wanafanya biashara ya mafuta wanamiliki vituo vya mafuta na wana mgongano,” alisema.

Kuhusu Christopher ole Sendeka, Lissu alidai kuwa amekuwa akizipigia debe kampuni tatu zilizonyimwa tenda ya kuiuzia mafuta TANESCO akiwashawishi wajumbe wa kamati kuwa serikali ilikiuka kanuni kuipa tenda Kampuni ya PUMA Energy.

Mbunge mwingine aliyetajwa ni Vicky Kamata wa Viti Maalumu ambaye alidaiwa kuwa na mgongano wa kimasilahi na Maswi.

“Tunampongeza Spika kwa kuivunja Kamati ya Nishati na Madini lakini tunataka azivunje pia zile za LAAC, inayoongozwa na Augustine Mrema (TLP) na POAC ya Zitto, kwa kuwa baadhi ya wajumbe wake wamekuwa wakitajwa sana kujihusisha na vitendo vya rushwa.

Fukuto la kutajwa kwa majina ya wabunge wanaotuhumiwa kwa rushwa lilitawala mjadala wa Bunge jana, ambapo wabunge, Kangi Lugora (Mwibara), James Mbatia (Kuteuliwa), Ali Keisy (Nkasi), Joshua Nassari (Arumeru Mashariki na Salum Baruani (Lindi Mjini), waliomba mwongozo wa Spika wakidai wahusika wawekwe wazi.

Hata hivyo, katika mwongozo wake, Naibu Spika, Job Ndugai, alisema kuwa Kamati ya Maadili, Haki na Madaraka ya Bunge inaendelea na uchunguzi kama ilivyoagizwa na Spika ndipo hatua nyingine zitafuata.

“Wabunge, baadhi mtaitwa kusaidia kamati hiyo lakini si kwamba ukiitwa kuhojiwa na kamati inamaanisha umepokea rushwa, ni katika hatua za mwanzo tu kufikia ukweli wa kile kinachochunguzwa. Labda niwaeleze kuwa Spika amekubali kuiangalia kamati hii ili wale wajumbe wenye mgongano wa kimasilahi waondolewe,” alisema.

Alikataa kutaja majina ya watuhumiwa akisema kuwa Spika pamoja na yeye hawawajui wahusika ndiyo maana wanachunguza kuwabaini. Lakini aligusia kuwa Taasisi ya Kuzuia na kupambana na Rushwa (TAKUKURU), imeanza kuwahoji baadhi ya wabunge.

Ndugai pia alitolea ufafanuzi mwongozo ulioombwa na Mbunge wa Tabora Mjini, Ismail Rage (CCM), aliyetaka kujua ni kwanini kiongozi wa upinzani alitaja majina ya watuhumiwa wa rushwa kutoka CCM wakati kwenye chama chake cha CHADEMA kuna watuhumiwa pia.

“Mimi ningewashauri kuwa katika jambo hili tuwe na subira na tukitaka kulizungumza tutende haki kwa pande zote, maana hakuna chama chenye sera ya kura rushwa, tusilifanye kisiasa kwa kuoneana,” alisema Ndugai.

Watuhumiwa wajitetea

Tanzania Daima iliwasiliana na watuhumiwa kujua wana kauli gani dhidi ya tuhuma hizo ambapo Mwijage, Msafiri na Munde simu zao ziliita pasipo kupokewa wakati Ole Sendeka, Kisangi na Nassir walizikanusha.

Nassir alisema kuwa si kweli kuwa anafanya biashara ya mafuta bali aliwahi kufanya kazi katika Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC) ambapo alipata ujuzi na hivyo kuwa na nia ya kutaka kuanza biashara ya gesi.

“Lissu ni mwanasheria lakini nashindwa kuelewa ni kwanini anafanya ‘generalization’ katika jambo hili, mimi sifanyi biashara ya mafuta na TANESCO wala serikali kupitia wizara husika, nampuuza kwa madai yake na nitamchukulia hatua,” alisema.

Kwa upande wake Kisangi alikiri kufanya biashara ya mafuta, akisema anamiliki vituo vya mafuta eneo la Mbagala Rangi Tatu, lakini akafafanua kuwa kila wakati alipochangia hoja ndani ya Bunge na kwenye Kamati ya Nishati na Madini alitangaza masilahi yake.

“Mimi niko vizuri sina wasiwasi, rejea kumbukumbu rasmi za Bunge utaona kuwa nimetangaza masilahi yangu, hivyo namshangaa huyu mwanasheria. Ina maana naye kuwa kwenye Kamati ya Sheria ni mgongano wa masilahi kwa vile ni mwanasheria?” alihoji.

Ole Sendeka naye alisema kuwa hakuwahi kuzipigia debe kampuni anazohusishwa nazo kwani alichokifanya kwenye kamati ni kuwaeleza wajumbe namna Maswi alivyovunja sheria ya manunuzi ya umma.

“Maswi ameichukua PUMA Energy kama mashati ya mitumba sokoni wala haikuwa kushindanishwa, sasa kama Lissu ambaye ni mwanasheria haoni hilo napata taabu,” alisema.

Source: Tanzania Daima 31 July 2012

Washirikishe Google Plus

About SeriaJr

SeriaJr will keep you updated with all current political news countrywide "Ndiye "Bosi" Mzito Arusha255" Karibu Tuhabarike!.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 maoni:

TANZANIA, THE HOME OF KILIMANJARO