Tunakusogezea karibu habari na matukio, zaidi habari za kisiasa na utawala, matukio ya Arusha na maeneo jirani, bila kusahau na mambo mengineyo ya kitaifa yanayojiri katika maeneo mbalimbali ya nchi kuhusu maendeleo na kuwa ya maslahi kwa watu wengi. Burudani na michezo pia havijasahaulika. Kizuri zaidi, unaweza kupata link ya Blogu nyingine na website muhimu hapa hapa kwa kuscroll mpaka chini. Karibu tuhabarike!

Aliyemteka Dk. Ulimboka atinga kortini

na Shehe Semtawa

RAI wa Kenya, Joshua Mulundi (21), jana alasiri alifikishwa kwa siri kubwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, akikabiliwa na makosa ya kumteka na kutaka kumuua Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, Dk. Steven Ulimboka.

Wakili wa serikali, Ladslaus Komanya, mbele ya Hakimu Agnes Mchome, alidai kuwa Mulundi ambaye mkazi yake ni Murang’a nchini Kenya, anadaiwa kuwa  Juni 26 mwaka huu, akiwa eneo la Leaders Club alimteka Dk. Ulimboka.

Katika shtaka la pili, Komanya alidai kuwa Juni 26 mwaka huu, akiwa katika eneo la Msitu wa Mwabepande Tegeta, Dar es Salaam, kinyume cha sheria, mshtakiwa huyo alijaribu kumsababishia kifo Dk. Ulimboka.

Hakimu Mchome alisema mshtakiwa hatakiwi kujibu chochote kwa sababu mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza shauri hilo, kwani Mahakama Kuu ndiyo yenye mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo.

Baada ya kusomewa mashtaka hayo Mulundi alidai kuwa kosa aliloshtakiwa nayo siyo sahihi.

Hata hivyo, Hakimu Mchome  alimwambia kuwa shauri hilo linasikilizwa Mahakama Kuu na siyo mahakamani hapo. Kesi imeahirishwa hadi Agosti 5 mwaka huu, itakapokuja kwa ajili ya kutajwa na mshtakiwa amerejeshwa rumande.

Juni 27 mwaka huu, Dk. Ulimboka aliokotwa na msamalia mwema katika msitu huo wa Mwabepande akiwa amejeruhiwa vibaya na kisha akafikishwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili akiwa na maumivu makali na kuanza kutibiwa.

Lakini hata hivyo, siku chache baadaye madaktari waliokuwa wakimtibu walisema wameshindwa kumtibu katika hospitali hiyo kwa sababu hakuna vifaa, hivyo wakamsafirisha kwenda nchini Afrika Kusini ambako hadi sasa anaendelea na matibabu.

Kova aleza alivyonaswa

Mapema Kamanda wa Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam, Suleiman Kova, alisema kuwa mtuhumiwa huyo Joshua Gitu Mhindi, ana kitambulisho cha utaifa Na.29166938 kilichotolewa Nyeri na hati ya kusafiria ya dharura Na.0123431 iliyotolewa Namanga Kenya.

Alisema kuwa katika mahojiano na polisi, mtu huyo alieza kwamba yeye ni mwanachama wa kikundi cha kihalifu kinachojulikana kama Gun Star chenye makao yake eneo la Ruiru Wilaya ya Thika nchini Kenya na kudai kuwa kinaongozwa na mtu mwenye jina la utani Silence akisaidiwa na Past, ambao wamekuwa wakifanya matukio mengi ya kihalifu nchini Kenya.

Kova alisema kuwa mtu huyo alipohojiwa zaidi alisema alikuja Tanzania na wenzake 12 kwa lengo la kumdhuru Dk. Stephen Ulimboka baaada ya kukodiwa na mtu ambaye hakumtaja jina, ambaye anaamini kuwa ni mtumishi wa serikali.

Madaktari waridhia maandamano

Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), kimesema maandamano yao yako pale pale na yatafanyika Jumatatu ya Julai 16, saa nne, na si vinginevyo.

Aidha, MAT, kimelaani kutekwa na kupigwa kwa mwenzao Dk. Steven Ulimboka na kufutiwa leseni kwa wanafunzi wa vitendo (interns).

Uamuzi huo wa MAT, ulitolewa jijini Dar es Salaam jana, katika kikao cha dharula cha madaktari 500 walioketi katika ukumbi Kituo cha Utamaduni wa Korea.

MAT, kupitia Katibu wake, Rodrick Kabangila alisema kuwa kwa pamoja wanalaani vitendo vya unyanyaswaji wa serikali dhidi yao, uamuzi wa Baraza la Madaktari (MCT) wa kuwafutia leseni wanafunzi wa vitendo bila kuwapa nafasi ya kuwasikiliza kutoa maelezo yao.

“MCT lilishindwa kuwaita na kupata maelezo yao badala yake walijichukulia hatua za haraka za kuwafukuza, wakati suala hilo lipo mahakamani,” alisema.

Kwa mujibu wa Kabangila, madaktari wanalaani hatua ya kunyimwa chakula na kufukuzwa na FFU kwenye vyumba vya kulala (hosteli), madaktari kabla ya taarifa ya maandishi kutoka wizarani.

Pia wanafunzi hao na wengine walinyimwa posho kabla ya barua ya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, kwamba vitendo hivyo na vingine vinaonyesha udhalilishwaji mkubwa kwao, ikizingatiwa kuwa ni wanataaluma wanaohitajika ndani ya nchi.

Katika maelezo yake, taaluma hiyo ina umuhimu mkubwa, na ikiwa unyanyasaji huo utaendelea, kutasababisha idadi kubwa ya madaktari kuondoka nje ya nchi.

Alionya kwamba endapo wataondoka taifa litakosa madaktari na kutafanya wananchi zaidi ya milioni 12 kukosa huduma ya afya.

Mbali na hilo, katibu huyo alisema bado milango iko wazi kukutana na serikali ili kukaa mezani kwa lengo la kumaliza mgogoro wao ambao umedumu kwa muda mrefu sasa.

Kimsingi, Kabangila alisema kutokana na hatua hizo, wameandaa maandamano pindi watakapopata kibali kutoka vyombo vya usalama.

Hata hivyo, alisema maandamano ni haki yao na kibali ni kwa ajili ya ulinzi wao; kwamba maandamano yana lengo la kupinga dhuluma na uonevu dhidi ya taaluma muhimu ya udaktari na madaktari wenyewe.

“Maandamano yataanzia nje ya Hospitali ya Taifa Muhimbili, tutaishia kwenye geti la Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, tukiwa na mabango ya kulaani kitendo cha kutekwa, kupigwa na kutelekezwa kwenye Msitu wa Pande alichofanyiwa Dk. Steven Ulimboka,” alisema.

Dk. Kabangila alisema kuwa wataishinikiza serikali iunde tume huru kwa ajili ya kuchunguza suala la Dk. Ulimboka itakayofanya kazi haraka na wahusika wote wafikishwe kwenye vyombo vya sheria.

SOURCE: TANZANIA DAIMA, 14 July 2012

Washirikishe Google Plus

About SeriaJr

SeriaJr will keep you updated with all current political news countrywide "Ndiye "Bosi" Mzito Arusha255" Karibu Tuhabarike!.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 maoni:

TANZANIA, THE HOME OF KILIMANJARO