Tunakusogezea karibu habari na matukio, zaidi habari za kisiasa na utawala, matukio ya Arusha na maeneo jirani, bila kusahau na mambo mengineyo ya kitaifa yanayojiri katika maeneo mbalimbali ya nchi kuhusu maendeleo na kuwa ya maslahi kwa watu wengi. Burudani na michezo pia havijasahaulika. Kizuri zaidi, unaweza kupata link ya Blogu nyingine na website muhimu hapa hapa kwa kuscroll mpaka chini. Karibu tuhabarike!

UGEUGEU NA UPAPARA WA KUPATA FEDHA UNAKWAMISHA VIJANA

_MG_1920

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Dk. Tausi Kida akiingia katika ukumbi wa mkutano hoteli ya Double Tree by Hilton kwa ajili ya warsha ya vijana na ajira iliyofadhiliwa na Mpango wa Shirika la Utafiti ya Maendeleo ya Kimataifa kutoka Canada (IDRC) na kuratibiwa na ESRF.

Na Mwandishi wetu

VIJANA nchini Tanzania wanatakiwa kujitambua, kuacha kuwa kigeugeu na kufanya papara ya kupata fedha kama wanataka kuendelea na kufanikiwa kibinafsi na kiuchumi.

Kauli hiyo imetolewea jana na Meneja Ajira za Kifundi kwa vijana na Mratibu Kazi wa Shirika la Kimataifa la Kazi (ILO) Dk. Annmarie Kiaga kwenye warsha ya wadau wa kitaifa ya kujadili suala la ajira kwa vijana Tanzania .

Kauli yake hiyo kwa vijana hao waliojumuika katika hoteli ya DoubleTree by Hilton, Dar es salaam, ilitokana na tafiti mbalimbali zilizofanyika nchini ambazo zinaonesha kwamba vijana wengi hawana msimamo wa maisha, hawana maono, hawana malengo binafsi wala kutambua matarajio.

Amesema: “ Usipojitambua, leo nikija nikakueleza habari za kuanzisha biashara ya matofali utachangamkia. Kesho akija mtu mwingine akakueleza kuhusu uchimbaji wa madini utaacha kutengeneza tofali na kukimbilia machimboni”.

Akizungumza kwa ufasaha kabisa kuhusu vijana na ajira, alisema kila mmoja ana nafasi yake katika kuleta maendeleo yake na taifa na kwamba lazima kujituma na si kubweteka na kulalamika tu.

Akizungumza kwa mfano alimzungumzia kijana mmoja Joseph ambaye alikuwa mwadilifu sana na mwenye kumwamini Mungu. Anasema Kila siku Joseph aliamka asubuhi na kumuomba Mungu amsaidie aondokane na umaskini alionao.

Alifanyakazi hivyo kwa miaka 30 lakini maombi yake hayakumsaidia kuondokana na umaskini.

Siku moja, alisema, Mungu alimuona Joseph akiwa na masikitiko makubwa akamuuliza kulikoni, Joseph akamjibu: “Mungu ni miaka 30 leo tangu nianzie kukuomba uniwezeshe nishinde bahati nasibu. Mimi nimeishi maisha yangu kwa uadilifu nawe wajua . Lakini mbona maombi hayatimii?”

_MG_1976

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Dk. Tausi Kida akifungua warsha ya vijana na ajira iliyofadhiliwa na Mpango wa Shirika la Utafiti ya Maendeleo ya Kimataifa kutoka Canada (IDRC). Kushoto ni Meneja Ajira za Kifundi kwa vijana na Mratibu Kazi wa Shirika la Kimataifa la Kazi (ILO) Dk. Annmarie Kiaga na kulia ni Kiongozi Mpango wa Ukuaji na Ajira wa Taasisi wa Mpango wa Shirika la Utafiti ya Maendeleo ya Kimataifa kutoka Canada (IDRC) Dk. Arjan de Haan.

Naye Mungu akatabsamu akamwambia, Joseph, si ununue tiketi basi?

Dk Kiaga alisema kwa kuzingatia hadithi yake kila mmoja anatakiwa kufanya kitu na Joseph alisahau kwamba huwezi kushinda bahati nasibu bila kununua tiketi.

“Kumbuka haitoshi kuwa na elimu na ujuzi kama hutaweza kuweka elimu hiyo au ujuzi ulionao katika vitendo” alisema na kuongeza kuwa Joseph alikuwa anajua anahaitaji fedha ya kianzio lakini hakuchukua hatua ya kupata hela hiyo.

Alisema pamoja na ukweli kuwa asilimia 40 ya watu wasio na ajira duniani ni vijana, kwa maana ya kwamba kuna vijana wapatao milioni 75 duniani kote wanatafuta ajira huku vijana wa kike wakiwa na changamoto kubwa zaidi, ipo shida kubwa ya vijana kukata tamaa.

Aidha alisema kwamba hali ya kukata tamaa imewapeleka vijana kuongezeka katika soko la vijana wanaopata kazi zisizo na staha.

Alisema pamoja na sera zilizopo vijana wanatakiwa kuwa na shauku na kazi na pia kujitambua.

“Vijana wa siku hizi hawana mitazamo sahihi kuhusu ajira. Kwamba vijana hawana shauku na kazi na wana mitazamo hasi (ili mradi kazi..mkono uende kinywani?) . Matokeo yake ni kwamba vijana hawatumii ubunifu wowote katika kuboresha uwezekano wao wa kupata kazi zenye staha” alisema.

Amesema mtaji unahitaji kujiboreshea seti ya ujuzi katika kutafuta kazi ikiwa ni pamoja na uwezo, uzoefu na elimu.

_MG_2014

Meneja Ajira za Kifundi kwa vijana na Mratibu Kazi wa Shirika la Kimataifa la Kazi (ILO) Dk. Annmarie Kiaga akizungumza kwenye warsha ya vijana na ajira iliyofadhiliwa na Mpango wa Shirika la Utafiti ya Maendeleo ya Kimataifa kutoka Canada (IDRC) na kuratibiwa na ESRF.

Alisisitiza kuwa vijana waliowengi hawajitambui na kujiuliza ‘mimi ni nani’ au hawana malengo binafsi na matarajio mimi nataka kuwa nani na kusema bila kuyafanyia kazi mambo hayo mawili ya shauku ya kazi na kujitambua hakutakuwepo na mabadiliko.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Dk Tausi Kida, akifungua warsha hiyo alisema pamoja na taifa kuwa mstari wa mbele kushughulikia ajira kwa vijana kwa kutunga sera zilizolenga kukidhi haja ya ajira,ikiwemo Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana ya mwaka 2007, Sera ya Taifa ya Ajira ya mwaka 2008 na na mpango wa utekelezaji wa sera ya taifa ya ajira kwa vijana iliyo chini ya mtandao wa ajira unaofadhiliwa na shirika la kazi la Umoja wa Mataifa, changamoto bado zipo.

Aliwataka washiriki wa warsha hiyo wakiwemo vijana waliofanikiwa kueleza siri za fursa na kujiajiri ili kutoa mwanga kwa wenzao.

Pamoja na warsha hiyo kutoa nafasi kwa vijana kujadili namna ya kutambua na kutumia fursa za kuichumi zilizopo nchini, kutoa ujuzi kwa vijana wa namna ya kuingia katika soko la ajira ikiwa ni pamoja na kujiajiri, kukuza ujasiriamali na kuendeleza biashara, Dk Kida aliwasihi vijana kujitafutia riziki yake na kushiriki ipasavyo katika shughuli za kiuchumi na maendeleo.

Aliwataka kujijengea uwezo wa kufanyakazi pamoja na kubaini na kuzitumia fursa za kiuchumi na kibiashara zilizopo nchini.

Warsha hiyo iliyofadhiliwa na Mpango wa Shirika la Utafiti ya Maendeleo ya Kimataifa kutoka Canada (IDRC) ilikutanisha vijana kutoka mikoa mbalimbali nchini Tanzania na kuwezeshwa kwa sehemu kubwa na Taasisi ya tamasha ambapo Mkurugenzi wake Mtendaji Richard Mabala alikuwa Mchokozaji mkuu.

Akiwasilisha salamu kutoka IDRC, kiongozi Mpango wa ukuaji na ajira wa taasisi hiyo. Dk Arjan de Haan alisema kwamba taasisi hiyo ya serikali ya Canada imekuwa ikitoa ushirikiano katika tafiti zilizolenga kuangalia utatuaji wa tatizo la ajira kwa namna inavyofaa.

_MG_2200

Mtafiti Mwandamizi ESRF, Dk. Georgina Ole Saibul akiwasilisha mada katika semina ya vijana na ajira.

Alisema kwamba kwa kawaida taasisi yake husaidia pale inapoona utafutaji wa mbinu za kutatua tatizo unashirikisha na wahusika ili kupata suluhu endelevu ya tatizo husika.

Alisema ameridhishwa na kuona kwamba warsha hiyo imezingatia kanuni za IDRC za kutaka kutatua tatizo la ajira kwa kushirikisha vijana wenyewe, kuangalia na kushauri namna bora ya kukabili tatizo la ajira ambao kwa sasa ni changamoto kubwa duniani.

Alisema kwamba ipo haja ya kubadili baadhi ya sera kulingana na mahitaji ya sasa ili kuwezesha vijana wengi zaidi kuingia katika soko la ajira.

Wakati wa utambulisho na kuelezea kero zao katika ajira wengi wa vijana waligusia kuwapo kwa sera ambazo si rafiki zinazotengeneza urasimu mkubwa katika kusaidiwa.

Ingawa wengi walisema fursa zipo, walizungumzia kutopata ushirikiano kutoka kwa wazazi , viongozi na taasisi mbalimbali zinazodai kupambana na ukosefu wa ajira kwa vijana.

Aidha vijana wengine walisema kwamba ni kweli kuna mtazamo hasi kwa vijana hasa kukata tamaa na pia kutaka maendeleo ya kasi huku wakikosa ubunifu.

Joachim Fanuel kutoka singida Youth Entrepreneurs and Consultants Cooperative Society (SYECLOS) alisema kwamba ingawa wao wanaendesha miradi ya kuku wa kienyeji na asali kama fursa zilizopo wanakabiliwa na tatizo la kukata tamaa kutokana na kuona kwamba inachukua muda mrefu kupata vitu wanavyotaka.

Aidha alisema kwamba wamekuwa hawasikilizwi na serikali na taasisi mbalimbali kwa kuwa hawana mali za kuwakilisha kama dhamana katika mambo mbalimbali.

 

_MG_2213

Johari A. Sadik kutoka kampuni inayotengeneza nguo za kitamaduni Binti Africa, akitoa ushuhuda kwamba vijana wanaweza kama watajitambua katika warsha ya siku mbili vijana na ajira inayofanyika hoteli ya DoubleTree by Hilton.

Kijana Musa Mohammed kutoka Zanzibar alisema kwamba japo wana fursa za usindikaji wa vyakula, mizizi na matunda wamekuwa na tatizo la ujuzi katika uchakataji, sera duni zisizojibu mahitaji yao na kuwalinda katika soko.

Binti mmoja kutoka Binti Africa Kampuni inayotengeneza nguo za kitamaduni alisema kwamba kuna shida ya kukata tamaa miongoni mwa vijana lakini pia hawajali kutafuta taarifa wanazohitaji wakisubiri kutafuniwa.

Vijana wengine walizungumzia ugumu wa mitaji, ukosefu wa taaluma na mfumo wa elimu kwuatengeneza kupata ajira katika serikali na taasisi zake.

Mshiriki Leticia Mango kutoka Kigoma alisema kwamba ipo shida ya vijana wenye vipaji ambao hawana elimu vijijini kudharaulika na kutothaminiwa kwa kile kinachoonekana sio wasomi.

Alisema vijana wasomi wakiunganika na wenye vipaji wanaweza kuwa mbali zaidi na kusisitiza ipo haja vijana kuwa pamoja kwa maendeleo yao.

_MG_2221

Joachim Fanuel kutoka Singida Youth Entrepreneurs and Consultants Cooperative Society (SYECCOS) akionesha chupa ya asali kutoka kwa mradi wa kikundi cha vijana ambao waliamua kujiajiri katika warsha ya vijana na ajira.

_MG_2220

Joachim Fanuel kutoka Singida Youth Entrepreneurs and Consultants Cooperative Society (SYECCOS) akizungumza na washiriki wa warsha ya vijana na ajira.

_MG_2178

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Dk. Tausi Kida (kushoto) akiwa na Kiongozi Mpango wa Ukuaji na Ajira wa Taasisi wa Mpango wa Shirika la Utafiti ya Maendeleo ya Kimataifa kutoka Canada (IDRC), Dk. Arjan de Haan wakiwa katika warsha ya vijana na ajira.

_MG_2226

Vijana wakishiriki kazi za vikundi kwenye warsha hiyo.

_MG_2229

_MG_2138

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Dk. Tausi Kida akiwa katika picha ya pamoja na vijana walioshiriki warsha ya vijana na ajira hoteli ya Double Tree by Hilton jijini Dar.

Washirikishe Google Plus

About Unknown

SeriaJr will keep you updated with all current political news countrywide "Ndiye "Bosi" Mzito Arusha255" Karibu Tuhabarike!.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 maoni:

TANZANIA, THE HOME OF KILIMANJARO