Tunakusogezea karibu habari na matukio, zaidi habari za kisiasa na utawala, matukio ya Arusha na maeneo jirani, bila kusahau na mambo mengineyo ya kitaifa yanayojiri katika maeneo mbalimbali ya nchi kuhusu maendeleo na kuwa ya maslahi kwa watu wengi. Burudani na michezo pia havijasahaulika. Kizuri zaidi, unaweza kupata link ya Blogu nyingine na website muhimu hapa hapa kwa kuscroll mpaka chini. Karibu tuhabarike!

IRELAND YAWAKABIDHI SCHOLARSHIP WATANZANIA 14 KUSOMEA SHAHADA YA UZAMILI

 Balozi wa Ireland nchini Tanzania, Bi. Fionnuala Gilsenan, akizungumzia kuhusu ufadhili kwa Watanzania wanaokwenda vyuo mbalimbali vya ndani na nje ya nchi. Sherehe hizo zimefanyika Alhamisi, Agosti 20, 2015 kwenye ofisi za ubalozi huo Masaki jijini Dar es Salaam. (Picha na habari na Daniel Mbega wa www.brotherdanny.com).

Baadhi ya wanufaika wa ufadhili huo wakimsikiliza Balozi wa Ireland (hayuko pichani).
 Baadhi ya wafanyakazi na wageni waalikwa wakimsikiliza Balozi Gilsenan.
 Deogratias Gabriel Rugarabamu, Ofisa Tabibu wa Wilaya ya Kilindi, akipokea cheti cha shukrani baada ya kuhitimu shahada ya uzamili ya Medical Entomology and Clinical Parasitology katika Chuo Kikuu cha Tumaini, KCMC .
Balozi Fionnuala Gilsenan wa Ireland akimpongeza Rubea Mohammed Ali, Mkuu wa Idara katika Wizara ya Kilimo na Maliasili, Zanzibar baada ya kuhitimu shahada ya uzamili katika Chuo Kikuu cha Sokoine katika Elimu ya Kilimo na Ushauri (Agricultural Education and Extension).
David Eliatosha Lekei, Ofisa Kilimo Wilaya ya Hai akipokea cheti cha shukrani kutoka kwa Balozi wa Ireland nchini, Bi.Fionnuala Gilsenan baada ya kuhitimu shahada ya uzamili kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine katika Elimu ya Kilimo na Ushauri (Agricultural Education and Extension).
 Mshereheshaji akisoma majina ya wanufaika.
Stella Zakayo Munisi, Meneja Rasilimali Watu na Utawala wa Shirika la Sikika, akipokea hati ya ufadhili kwenda kusomea shahada ya uzamili kuhusu Organizational Development and Change katika Chuo Kikuu cha Dublin, Ireland. 

Na Daniel Mbega
SERIKALI ya Ireland kupitia Ubalozi wake nchini Tanzania, leo Agosti 20, 2015 imekabidhi scholarship kwa Watanzania 14 ambao watakwenda kusomea kozi mbalimbali za shahada ya uzamili (masters) ambapo wanne kati yao wakienda kusoma vyuo vikuu nchini Ireland.
Akikabidhi hati hizo za ufadhili wa masomo, Balozi wa Ireland nchini Tanzania, Bi. Fionnuala Gilsenan, alisema utaratibu wa kutoa ufadhili kwa wataalamu mbalimbali ni jambo la msingi kutokana na ukweli kwamba ujuzi watakaoupata unaweza kuliletea taifa maendeleo.
“Ufadhili huu ni sehemu ya Mpango wa Mafunzo wa Kila Mwaka (Fellowship Training Programme), katika sukuma mbele maendeleo ya nchi washirika wetu, tunadhani tunao wajibu wa kusaidia pia kuwaelimisha watalaamu wao,” alisema.
Aliwataja wanufaika wanne waliobahatika kwenda ng’ambo kuwa ni Stella Zakayo Munisi, Meneja Rasilimali Watu na Utawala wa Shirika la Sikika, ambaye anakwenda kusomea shahada ya uzamili (Organizational Development and Change) na Cosmas Joseph Mworia, Ofisa Ushirika na Ofisa Ufuatiliaji na Ukadiriaji katika Kilimo wa Halmashauri ya Wilaya Kondoa anayekwenda kusomea shahada ya uzamili katika Kilimo Endelevu na Maendeleo Vijijini (Sustainable Agriculture and Rural Development). Wawili hao wanakwenda katika Chuo Kikuu cha Dublin.
Flavian Majenga Lihwa, Mratibu Programu ya Elimu wa Shirika la Care Tanzania yeye anakwenda Chuo Kikuu cha Dublin Institute of Technology kuchukua shahada ya uzamili katika Maendeleo Endelevu (Sustainable Development) na Zabron Elias Masatu, Mganga Mkuu wa Wilaya (DMO) ya Misenyi yeye anakwenda Chuo Kikuu cha Taifa cha Ireland Maynooth (NUIM) kuchukua shahada ya uzamili ya Immunolojia na Afya (Immunology and Global Health).
Wanufaika wengine 10 wa mwaka huu, kozi na vyuo wanavyokwenda vikiwa kwenye mabano ni, Siwajibu Ally Selemani Malenge, Kaimu Ofisa Kilimo/Umwagiliaji na Ushirika wa Wilaya ya Kigoma (Chuo Kikuu cha Sokoine – Elimu ya Kilimo na Ushauri ‘Agricultural Education and Extension’); Edita Byangwamu Rutatora Kokwijuka, Ofisa Kilimo Daraja la Kwanza kutoka Wilaya ya Muheza (Chuo Kikuu cha Sokoine – Kilimo); Doreen Elias Mangesho, Mhasibu Mkuu wa CCBRT (Chuo Kikuu cha Dar es Salaam – Utawala wa Fedha); Elinlaa Michael Kivaya, Mchumi wa Kilimo wa Wilaya ya Ngorongoro (Chuo Kikuu cha Sokoine – Kilimo na Uchumi Mtambuka ‘Agriculture and Applied Economics’); na Joshua Julius Musimu, Mkufunzi wa Kilimo Daraja la Pili kutoka Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika (Chuo Kikuu cha Sokoine – Uchumi wa Kilimo ‘Agricultural Economics’).
Wengine ni Fredrick Pius Massawe, Ofisa Kilimo Daraja la Kwanza kutoka Ofisi ya Katibu Tawala Mkoa wa Kilimanjaro (Chuo Kikuu cha Sokoine –Kilimo); Samuel Korinja Olekao, Mratibu wa Kinnapa Development Programme (Chuo Kikuu cha Sokoine – Utunzaji wa Maliasili na Kilimo Endelevu); Eva Emmanuel Mbambale, Ofisa Program wa Sikika (Chuo Kikuu cha Makerere,Uganda – Afya ya Jamii); Iddi Alfani Shekabugi, Mchumi Daraja la Kwanza katika Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika (Chuo Kikuu cha Mzumbe – Uchumi na Fedha kwa Maendeleo); na Felix Lyope Lubuga, Ofisa Utafiti wa Taasisi ya Afya Ifakara (Chuo Kikuu cha Dar es Salaam – Afya ya Jamii).
Awali, Balozi Fionnuala aliwatunuku vyeti wanufaika wengine 10 waliomaliza mwaka 2013 na 2014 katika fani mbalimbali.
Hao ni Deogratias Gabriel Rugarabamu, Ofisa Tabibu wa Wilaya ya Kilindi (Chuo Kikuu cha Tumaini, KCMC – Medical Entomology and Clinical Parasitology);  Pudensiana Clement Panga, Ofisa Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi (Chuo Kikuu cha Sokoine – Sayansi ya Chakula); Fatma Ally Mwasola Libaba, Ofisa Utafiti (Lishe) kutoka Taasisi ya Chakula na Lishe (Chuo Kikuu cha Sokoine – lishe ya Binadamu); Rubea Mohammed Ali, Mkuu wa Idara katika Wizara ya Kilimo na Maliasili, Zanzibar (Chuo Kikuu cha Sokoine – Elimu ya Kilimo na Ushauri ‘Agricultural Education and Extension’); na David Eliatosha Lekei, Ofisa Kilimo Wilaya ya Hai (Chuo Kikuu cha Sokoine – Elimu ya Kilimo na Ushauri ‘Agricultural Education and Extension’).
Wengine waliohitimu mwaka 2014 ni John Nobert Kirway, Mkufunzi Mkuu wa Mifugo wa Wizara ya Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi, Arusha (Chuo Kikuu cha Sokoine –Tropical Animal Production); Teddy Frederick Dionis Mamboleo, Ofisa Utafiti (Lishe) kutoka Taasisi ya Chakula na Lishe (Chuo Kikuu cha Sokoine – Lishe ya Binadamu); Adam Khamis Haji, Ofisa Mipango na Utawala, Wizara ya Kilimo na Maliasili, Zanzibar (Chuo Kikuu cha Sokoine – Maendeleo Vijijini); Jacob Polycarp Ngowi, Mkufunzi wa Masuala ya Mifugo kutoka Wizara ya Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi (Chuo Kikuu cha Sokoine –Tropical Animal Production); na Mussa Said Bakari, Meneja wa Maeneo Tengefu – Pemba kutoka Wizara ya Kilimo na Maliasili, Zanzibar (Chuo Kikuu cha Sokoine – Utunzaji wa Maliasili na Kilimo Endelevu).
Mpango huo wa Mafunzo wa kila Mwaka unahusisha Mfuko wa Misaada wa Ireland (Irish Aid) kupitia program ya maendeleo ya Ubalozi huo nchini Tanzania.
Wanufaika wa mpango huo wameteuliwa na washirika wa maendeleo wa Ireland nchini Tanzania, zikiwemo wizara mbalimbali za Serikali, halmashauri za wilaya na mashirika yasiyo ya kiserikali, ambayo shughuli zao zinawiana na maeneo ya vipaumbele vya Irish Aid, hususan Kilimo, Afya, Lishe na Utawala.
Aidha, wanufaika wote ni watendaji wa kati ambao baada ya kuhitimu masomo yao watarejea kwenye mashirika na taasisi zao kutumia ujuzi walioupata kwa manufaa ya jamii.
“Kwa wanufaika watakaokwenda kusoma nchini Ireland, program inatoa fursa nzuri ya kujifunza katika hadhi ya kimataifa na kunufaika na hazina kubwa ya nyenzo za tafiti zinazotolewa kwenye Vyuo Vikuu na Taasisi za Teknolojia za Ireland,” amesisitiza Balozi Fionnuala.
Akaongeza: “Inatarajiwa kwamba mafunzo ya wataalamu hawa yatachangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya Tanzania, na kuendelea kuimarisha ushirika wa kielimu baina ya Ireland na Tanzania.”

Ireland, kupitia Mfuko wa Misaada (Irish Aid), imekuwa ikidhamini Mpango huo wa Mafunzo nchini Tanzania kwa miaka 40 sasa ambapo program hiyo imekuwa msingi wa msaada katika kuzijengea uwezo nchi zinazoendelea na inaendana na mkakati wa kupunguza umaskini wa nchi washirika wa Ireland, hasa lengo likiwa kuwapatia wataalamu elimu ya juu ili waendeleze taasisi zao.
(Imeandaliwa na www.brotherdanny.com. Simu 0656-331974)

PICHA ZAIDI TAZAMA HAPA
Washirikishe Google Plus

About Unknown

SeriaJr will keep you updated with all current political news countrywide "Ndiye "Bosi" Mzito Arusha255" Karibu Tuhabarike!.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 maoni:

TANZANIA, THE HOME OF KILIMANJARO