Tunakusogezea karibu habari na matukio, zaidi habari za kisiasa na utawala, matukio ya Arusha na maeneo jirani, bila kusahau na mambo mengineyo ya kitaifa yanayojiri katika maeneo mbalimbali ya nchi kuhusu maendeleo na kuwa ya maslahi kwa watu wengi. Burudani na michezo pia havijasahaulika. Kizuri zaidi, unaweza kupata link ya Blogu nyingine na website muhimu hapa hapa kwa kuscroll mpaka chini. Karibu tuhabarike!

Taarifa mbalimbali za TFF Kwa Vyombo Vya Habari Agosti 31, 2012

 

                                          Release No. 139
                              TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
                                             Agosti 31, 2012


MTIHANI WA MAWAKALA WA WACHEZAJI SEPT 27
Mtihani kwa ajili ya watu wanaotaka kuwa mawakala wa wachezaji wanaotambuliwa na Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) utafanyika Septemba 27 mwaka huu saa 4 kamili asubuhi ofisi za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

Kwa wanaotaka uwakala huo wanatakiwa kujisajili ambapo watapewa kanuni mbalimbali za FIFA na TFF ili waweze kujiandaa kikamilifu kwa mtihani huo utakaokuwa na sehemu mbili. Sehemu ya kwanza ni maswali kutoka FIFA wakati nyingine ni kutoka TFF. Ada ya mtihani ni dola 50 za Marekani.

Pia Damas Ndumbaro na Ally Mleh wa Manyara Sports Management ambao tayari ni mawakala wanaotambuliwa na FIFA wanatakiwa kufanya mtihani huo kama wanataka kuendelea na uwakala kwa vile muda wa leseni zao za awali umemalizika.

Mawakala wengine ambao ni John Ndumbaro, Mehdi Remtulla, Ally Saleh, Yusuf Bakhresa na Said Tully leseni zao bado ziko hai.

WACHEZAJI 17 WAPINGWA KWENYE USAJILI
Klabu mbalimbali zimewasilisha pingamizi Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kupinga usajili wa wachezaji 17 walioombewa usajili katika timu za Ligi Kuu.

Toto Africans ya Mwanza imewawekea pingamizi wachezaji Enyinna Darlinton aliyeombewa usajili Kagera Sugar, na Mohamed Soud anayekwenda Coastal Union kwa maelezo kuwa bado ina mikataba na wachezaji hao.

Pia Flamingo ya Arusha inapinga usajili wa wachezaji wake Kelvin Friday Iddy katika timu za Azam na Salim Walii (Polisi Mara) kwa vile taratibu za kuwahamisha bado hazijafanywa. Nayo Kagera Sugar inapinga usajili wa beki David Charles Luhende kwenda Yanga kwa vile ada ya uhamisho haijalipwa.

Super Falcon ya Chanjamjawiri, Chakechake, Pemba inapinga wachezaji wake wanne; Edward Christopher Shija, Samir Said Luhava (Simba), Robert Joseph Mkhotya (African Lyon) na Sultan Juma Shija (Coastal Union) kusajiliwa katika timu hizo kwa maelezo taratibu halali za uhamisho hazikufuatwa.

Mchezaji Othman Hassan aliyeombewa usajili Coastal Union anapingwa na Oljoro JKT kwa vile bado ana mkataba na timu hiyo unaomalizika Mei 24, 2013. Nayo Rollingstone Multipurpose Ateclass Foundation ya Arusha inapinga usajili wa Kigi Makassy kutoka Yanga kwenda Simba hadi itakapolipwa fidia ya kumlea mchezaji huyo kwa vile bado hajafikisha umri wa miaka 23.

Azam inapinga usajili wa Ramadhan Chombo ‘Redondo’ kwenda Simba kwa maelezo bado ina mkataba naye unaomalizika Juni 11 mwakani. Nayo Simba inapinga Kelvin Yondani kusajiliwa Yanga kwa maelezo kuwa ina mkataba naye uliosainiwa Desemba 23 mwaka jana.

Vilevile Simba imewasilisha malalamiko ya mchezo usio wa kiungwana katika usajili wa Mbuyu Twite aliyeko Yanga kwa maelezo alisaini mkataba na klabu yao Agosti Mosi mwaka huu mbele yao, viongozi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Rwanda (FERWAFA) na APR ambapo alilipwa dola 30,000 na nyingine 2,000 ikiwa ni fedha ya kujikimu na nauli yake ya kujiunga na klabu hiyo.

Nayo Yanga inapinga Simba kuwaacha wachezaji Dan Mrwanda, Haruna Shamte, Kanu Mbiyavanga na Lino Masombo kwa maelezo walishapatiwa leseni za kucheza Ligi ya Tanzania walizozitumia kwenye mashindano ya Kombe la Kagame. Pia inapinga Ramadhan Chombo ‘Redondo’ kujiunga Simba kwa vile ana leseni ya kuchezea Azam kwa msimu wa 2012/2013.

Pingamizi lingine la Yanga kwa Simba ni kuwa imezidisha idadi ya wachezaji wa kigeni wanaotakiwa kusajiliwa kwa maelezo inao wanane wakati wanaoruhusiwa ni watano. Imewataja wachezaji hao kuwa ni Lino Masombo, Felix Sunzu, Emmanuel Okwi, Mussa Mude, Kanu Mbiyavanga, Pascal Ochieng, Komalmbil Keita na Daniel Akuffor.

Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya TFF chini ya Mwenyekiti wake Alex Mgongolwa inatarajia kukutana Jumapili (Septemba 2 mwaka huu) kupitia pingamizi hizo pamoja na usajili wa wachezaji kwa ujumla kwa 2012/2013.

LIGI KUU TANZANIA BARA 2012/2013
Michuano ya Ligi Kuu kuwania ubingwa wa Tanzania Bara kwa msimu wa 2012/2013 itaanza Septemba 15 mwaka huu kwa timu zote 14 kujitupa kwenye viwanja tofauti.

Mechi za ufunguzi zitakuwa kati ya Simba vs African Lyon (Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam), Polisi Morogoro vs Mtibwa Sugar (Jamhuri, Morogoro), Tanzania Prisons vs Yanga (Sokoine, Mbeya), Mgambo JKT vs Coastal Union (Mkwakwani, Tanga), JKT Ruvu vs Ruvu Shooting (Azam Complex, Dar es Salaam), Kagera Sugar vs Azam (Kaitaba, Bukoba) na Toto Africans vs Oljoro JKT (Kirumba, Mwanza).

Mzunguko wa kwanza (first round) utamalizika Novemba 11 mwaka huu ambapo kwenye mzunguko huo mechi ya watani wa jadi Yanga na Simba itachezwa Oktoba 3 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Ligi hiyo itamalizika Mei 18 mwakani kwa mechi kati ya Toto Africans vs Ruvu Shooting (Kirumba), Mgambo JKT vs African Lyon (Mkwakwani), JKT Ruvu vs Mtibwa Sugar (Azam Complex), Tanzania Prisons vs Kagera Sugar (Sokoine), Simba vs Yanga (Uwanja wa Taifa), Oljoro JKT vs Azam (Sheikh Amri Abeid Kaluta) na Polisi Morogoro vs Coastal Union (Jamhuri).

Endapo Simba na Azam hazitafanikiwa kuvuka hatua mojawapo ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika na Kombe la Shirikisho, ratiba hiyo itafanyiwa marekebisho.
MECHI YA UFUNGUZI WA MSIMU WA LIGI 2012/2013

Mechi ya Ngao ya Jamii (Community Shield) kuashiria ufunguzi rasmi wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2012/2013 kati ya bingwa mtetezi Simba na makamu bingwa Azam itachezwa Septemba 11 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

SERENGETI BOYS KUJIPIMA KWA ASHANTI
Timu ya Taifa ya vijana wenye umri chini ya miaka 17 (Serengeti Boys) iliyokuwa kambini kujiandaa kwa mechi dhidi ya Kenya itavunja rasmi kambi yake kesho (Jumamosi) kwa mechi ya kirafiki dhidi ya Ashanti United.

Mechi hiyo dhidi ya Ashanti United iliyoko daraja la kwanza itachezwa kuanzia saa 10 jioni Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam kwa kiingilio cha sh. 2,000.

Serengeti Boys ilikuwa Septemba 9 mwaka huu icheze na Kenya kwenye mechi ya raundi ya kwanza ya michuano ya Afrika kwa vijana chini ya miaka 17, lakini Kenya ikajitoa ambapo sasa itacheza na Misri katika raundi ya pili. Mechi ya kwanza itachezwa Oktoba 14 mwaka huu jijini Dar es Salaam.

Mwishoni mwa Septemba, Serengeti Boys itarejea tena kambini kujiandaa kuikabili Misri ambapo kabla inatarajia kupata mechi ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya timu itakayotangazwa baadaye.
MCHEZAJI WA MTIBWA SUGAR NAYE APATA ITC

Shirikisho la Vyama vya Mpira wa Miguu Uganda (FUFA) limetuma Hati ya Uhamisho wa Kimataifa (ITC) kwa ajili ya mchezaji Ayoub Hassan Isiko aliyejiunga na Mtibwa Sugar akitokea timu ya Bull FC ya nchini humo.

ITC hiyo ilitumwa jana (Agosti 30 mwaka huu), hivyo kufanya wachezaji ambao ITC hazijapatikana hadi sasa kubaki wawili tu. Dirisha la usajili wa wachezaji litafungwa rasmi Septemba 4 mwaka huu.

Wachezaji ambao ITC zao bado hazijapatikana ni Salum Kinje na Pascal Ochieng kutoka AFC Leopards ya Kenya waliojiunga na Simba. ITC hizo zinatarajiwa kupatikana wakati wowote kwani tayari Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limeshaziomba kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Kenya (FKF) baada ya nyaraka zote zilizokuwa zikitakiwa kupatikana.
Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Washirikishe Google Plus

About SeriaJr

SeriaJr will keep you updated with all current political news countrywide "Ndiye "Bosi" Mzito Arusha255" Karibu Tuhabarike!.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 maoni:

TANZANIA, THE HOME OF KILIMANJARO