Tunakusogezea karibu habari na matukio, zaidi habari za kisiasa na utawala, matukio ya Arusha na maeneo jirani, bila kusahau na mambo mengineyo ya kitaifa yanayojiri katika maeneo mbalimbali ya nchi kuhusu maendeleo na kuwa ya maslahi kwa watu wengi. Burudani na michezo pia havijasahaulika. Kizuri zaidi, unaweza kupata link ya Blogu nyingine na website muhimu hapa hapa kwa kuscroll mpaka chini. Karibu tuhabarike!

Ukweli kuhusu masaibu ya Kibanda • Jicho lake lilipigwa risasi, madaktari waling’oa

WAKATI hali ya Mhariri Mtendaji wa Kampuni ya New Habari (2006) Limited, Absalom Kibanda ikiendelea kuwa tete, ukweli kuhusu afya yake na masaibu yaliyompata umejulikana, Tanzania Daima Jumapili limebaini.

Habari kutoka nchini Afrika Kusini kwenye Hospitali ya Milpark anakotibiwa, zinasema kuwa majeraha aliyoyapata baada ya kuvamiwa na watu wasiojulikana ni makubwa na yatamwacha na ulemavu wa kudumu.

Taarifa kutoka kwa watu walio karibu na Kibanda hospitalini hapo, zinasema kuwa mishipa yote inayozunguka jicho lake la kushoto imevunjika na jicho hilo limesambaratika lote na madaktari sasa, wameamua kuling’oa kabisa.

Madaktari wanne wanaomfanyia uchunguzi na kumpatia tiba Kibanda, wanasema kuwa jicho hilo limesambaratishwa na risasi na atawekewa jicho la bandia ambalo hata hivyo halitaweza kuona.

Kwa mujibu wa uchunguzi wa awali wa madaktari, kuna madhara kidogo kwenye ubongo wake na kiasi fulani cha damu kimechuruzika kwenye sehemu hiyo ya ubongo.

“Ubongo umedhurika kidogo na madaktari wanampa dawa ya kuyeyusha damu kwenye ubongo. Madaktari wanasema tusiogope, wanaweza kuidhibiti hali hiyo, lakini kipaumbele chao cha kwanza ni jicho. Wakishamaliza jicho ndipo watashughulikia ubongo,” ilisema taarifa hiyo.

Habari zaidi kuhusu afya ya mhariri huyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri nchini (TEF), zinasema kuwa jana alifanyiwa upasuaji kwa saa nne kwa ajili ya kutengeneza upya sura yake, kuweka vizuri paji la uso, na kurekebisha mfumo wa meno.

Pia alifanyiwa upasuaji wa jicho la kushoto na taarifa mbaya ni kwamba madaktari wameshindwa kuliokoa, hivyo wameling’oa.

Taarifa iliyotolewa jana na Katibu wa TEF, Neville Meena, ilisema kuwa madaktari wamechukua hatua ya kitatibu baada ya kuwa tayari jicho hilo lilikuwa limepondeka kwa ndani hivyo lisingeweza tena kuona. Atawekewa jicho la bandia la plastiki ambalo hata hivyo halitakuwa likiona.

“Jambo la kumshuruku Mungu ni kwamba kwa ujumla upasuaji huo uliochukua saa 5 na dakika 30 umefanyika kwa ufanisi mkubwa, na ulikuwa ukiongozwa na madaktari bingwa watatu. Wawili kati yao ni wataalamu wa kichwa na mmoja ni mtaalamu wa macho,” alisema Meena.

Katika upasuaji huo, hakukuwa na madhara ya ndani katika kichwa chake, hivyo kiko salama. Sura yake imejengwa upya kutokana na majeraha ambayo yalikuwa yametapakaa baada ya kupigwa na watu wasiojulikana.

Kwa mujibu wa habari hizo, changamoto kubwa waliyokutana nayo madaktari waliomfanyia upasuaji ni kurejesha katika sehemu yake baadhi ya mifupa midogo inayozunguka jicho, pia kurejesha taya la kushoto ambalo lilikuwa limeathiriwa na tukio la kupigwa kwake. Hata hivyo hatimaye walifanikiwa.

Ripoti kamili kuhusu upasuaji huo inatarajiwa kutolewa leo.

“Tuendelee kumwombea Mwenyekiti wetu Kibanda ili Mungu amponye. Kwa niaba ya Bodi ya Wakurungezi ya Jukwaa la Wahariri, kwa mara nyingine tunampa pole Kibanda pamoja na familia yake na tunamtakia uponyaji wa haraka,” ilisema taarifa hiyo.

Kabla ya upasuaji wa jicho jana, juzi Kibanda alifanyiwa upasuaji kutengeneza upya sura yake, kuweka vizuri paji la uso, na kurekebisha mfumo wa meno.

Upasuaji huo ulifanyika baada ya kupungua kwa majeraha na uvimbe katika sehemu mbalimbali za mwili wake, hususan kichwani na usoni.

Upasuaji huo pia unazingatia matokeo ya uchunguzi uliofanywa kwa zaidi ya saa 48 na jopo la madaktari wanne na kubaini madhara ya awali aliyoyapata mwanahabari huyo nguli.

Kuhusu jicho lake la kushoto ambalo lilijeruhiwa kwa kiasi kikubwa, madaktari walisema wangetoa uamuzi kuhusu aina ya upasuaji ambao wangeufanya baada ya kubaini hali halisi wakati watakapokuwa wakijenga sura yake ambayo iliharibiwa kwa majeraha.

“Wakati akipelekwa kwenye chumba cha upasuaji, Kibanda alikuwa akilalamikia maumivu kutokana na kidonda kilichopo kwenye mguu wake wa kushoto, kidonda hicho pia ni matokeo ya unyama aliyofayiwa,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo ya TEF.

Wakati Kibanda akiendelea na matibabu, jana Rais Jakaya Kikwete na Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana ambao wako Afrika Kusini kikazi, walimtembelea kumjulia hali hospitalini hapo.

Katika salamu zake, Rais Kikwete alisema serikali itawasaka hadi kuwatia nguvuni wahusika wa tukio hilo la utesaji na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.

Jinsi alivyoshambuliwa

Ingawa uchunguzi wa shambulio dhidi ya mhariri huyo umeanza, duru za uchunguzi zinasema kuwa kuna uwezekano mkubwa wa kundi lililohusika kuwa lile liliomteka, kumtesa na kisha kumtelekeza kwenye Msitu wa Mabwepande, Dk. Steven Ulimboka.

Dk. Ulimboka ambaye ni kiongozi wa Jumuiya ya Madaktari, aliyeongoza mgomo wa wanataaluma hao, aling’olewa meno, kucha, kupigwa kichwani - staili ya utesaji ambayo pia imetumika kwa Kibanda.

“Ukiangalia jinsi alivyoteswa Kibanda, hakuna tofauti na Ulimboka. Tofauti yake kidogo ni kwamba kwa Kibanda walitumia muda mfupi sana, kama dakika tano hivi. Lakini yote kwa yote, hawa ni watu hatari na ni wataalamu,” alisema mtoa habari wetu kutoka Jeshi la Polisi.

TMF watoa ruzuku kuchunguza

Katika hatua nyingine Mfuko wa Vyombo vya Habari Tanzania (TMF), umesema utatoa ruzuku ya fedha kuwawezesha waandishi wa habari kufanya habari za uchunguzi kubaini chanzo cha ukatili aliofanyiwa Kibanda.

Mkurugenzi wa TMF, Ernest Sungura katika taarifa yake alisema kuna kila sababu ya kuchunguza tukio hilo ambalo ni mfululizo wa matukio yanayopunguza uhuru wa vyombo vya habari nchini na kuwajengea woga wa kufanya kazi zao.

“Kwa vyovyote vile na kwa sababu zozote, wanaotoa vitisho kwa waandishi na kuwafanyia vitendo vya kikatili ni maadui wa uandishi wa habari za uchunguzi. Ni kwa msingi huu, TMF ipo tayari kutoa ruzuku ya chapuchapu na kuungana na wadau wengine wa habari kuchunguza kilichomtokea Kibanda,” alisisitiza Sungura katika taarifa hiyo.

Alisema TMF katika awamu ijayo, itaandaa mpango mkakati unaolenga kuwalinda waandishi wa habari wanaofanya habari za uchunguzi, ikiwemo kufikiria uwezekano wa kuwawekea bima ya kazi kwenye mazingira hatarishi.

Kibanda alivamiwa na kushambuliwa na watu wasiojulikana nyumbani kwake saa 6.15 usiku wa kuamkia Jumatano iliyopita, maeneo ya Goba Kunguru, Mbezi Beach, Kata ya Kawe, jijini Dar es Salaam.

Tayari Jeshi la Polisi limeunda tume, huku Jukwaa la Wahariri, nalo limeunda timu maalumu kuchunguza na kubaini waliohusika na tukio hilo.

Tanzania Daima, Machi 10, 2013; Picha na Global Publishers Ltd

Gazeti la Mtanzania likaripoti Machi 10, 2013 kuwa

Kibanda aliteswa na majasusi

Rais Jakaya Kikwete na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, wakimjulia hali Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania, Absalom Kibanda, akiwa hospitalini Afrika Kusini

SASA kuna dalili zinazoonyesha kuwa utekelezaji wa mpango wa kumteka na kumtesa kinyama Mhariri Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya New Habari (2006) Ltd, Absalom Kibanda, ulifanywa na watu waliopata mafunzo wanayopewa maofisa Usalama wa Taifa, Makachero wa Jeshi au wale wa Polisi, Mtanzania Jumapili linaripoti.

Duru za uchunguzi za Mtanzania Jumapili zimebaini kuwa ni watu wenye mafunzo maalumu ya kutesa na kuua, waliyopata katika vyuo vya kijasusi wenye uwezo wa kutekeleza kwa ufanisi utesaji wa aina aliyofanyiwa Kibanda au ule wa awali uliotekelezwa kwa aliyekuwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, Dk. Steven Ulimboka.

Makachero kadhaa waliobobea, waliozungumza na gezeti hili kuhusu aina ya mateso ambayo yamepata kutolewa kwa baadhi ya Watanzania (akiwemo Kibanda) na kundi la watu ambalo hadi sasa halijafahamika, walieleza kuwa kwa ufahamu wa kazi yao ya ukachero, watu waliomteka na kumtesa Kibanda ni ama maofisa usalama, Makachero wa Jeshi au Polisi au watu waliopata mafunzo yanayolingana na watu wa kada hizo.

Walisema wanaamini hivyo kwa sababu staili iliyotumika kumteka na kisha kumtesa, muda uliotumika kutekeleza utekaji na utesaji ni ule unaofundishwa katika vyuo vya kijasusi vilivyoko katika nchi za Magharibi na Asia ambavyo ni maalumu kwa ajili ya maofisa wa kijeshi na wale wa usalama.

Kachero mwingine mstaafu aliyeulizwa kuhusu aina hiyo ya kuteka na kutesa alisema ni jambo lililo wazi kuwa watu ambao wamekuwa wakitekeleza unyama huo wana mafunzo ya kazi hiyo ambayo hutolewa kwa watu maalumu hususan maofisa usalama na wanajeshi.

Alisema staili iliyotumika kumteka na kumtesa aliyekuwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, Steven Ulimboka, ndiyo iliyotumika kwa asilimia 95 kwa Kibanda, ambayo kwa mwana usalama yeyote, akisimuliwa au kumuona mtu aliyeteswa kwa namna hiyo, anajua kazi hiyo imefanywa na watu wa aina gani.

“Jambazi wa kawaida au mtu mwingine tu aliyeamua kufanya unyama siyo rahisi kwake kung’oa meno, kunyofoa kucha, kukata vidole, kuvunja mishipa na kutoboa macho bila kuwa na utaalamu wa kufanya kazi hiyo kwa wepesi na ufanisi kama inavyotokea sasa.

“Anaweza akafanya hivyo lakini si kwa ufanisi kama ilivyo kwenye matukio ya Kibanda na Ulimboka. Unajua, kuna mambo ambayo yako wazi, kazi za kitaalamu zinajulikana kuwa zimefanywa kitaalamu na za kienyeji nazo zinajulikana. Haya mambo yanafanywa na watu wenye ujuzi wa kazi hiyo, sasa hatujui ni akina nani, lakini ukweli unabaki hivyo kuwa watu hawa wana utaalamu wa kutesa na kuua,” alisema.

Utafiti iliofanywa na Mtanzania Jumapili umeonyesha kuwa makachero wa mashirika makubwa ya kijasusi duniani na hasa wa Nchi za Magharibi na zile za kikomunisti, hutesa watu waliowakusudia kwa sababu mbalimbali kwa staili kama aliyoteswa nayo Kibanda na Ulimboka.

Mateso ya aina hii hutolewa kwa watu wanaolazimishwa kutoa taarifa za siri au kukiri jambo walilolificha moyoni.

Kwa mujibu wa mtandao wa plisonplanet.com, utesaji wa kukata viungo vya binadamu hutekelezwa ili kumlazimisha mtu atoe taarifa au akiri jambo analolificha na kwamba hata baadhi ya mataifa ya Asia na Afrika hutumia mbinu hizi yalizozipata kutoka Nchi za Asia na Magharibi.

Taarifa za utesaji wa aina hiyo zilizo katika mitandao mbalimbali inayofuatilia mienendo ya kiintelijensia zinaeleza kuwa staili hiyo ya kinyama kutekelezwa kwa binadamu (slow slicing) na ilianzia nchi ya China katika miaka ya 600 AD hadi mwaka 1905 ilipokatazwa. Hata hivyo, inabainishwa kuwa mateso ya aina hiyo bado yapo katika baadhi ya nchi, zikiwemo za Afrika zinazotajwa kuongozwa kidikteta.

Sehemu ya taarifa iliyo katika tovuti hiyo inasomeka kuwa; ‘katika mateso ya aina hii, mtesaji hutumia kisu chenye ncha kali kutoa jicho, kung'oa au kukata masikio, pua, ulimi, vidole, na kabla ya kuendelea na hivyo hukata vipande vidogo vya nyama kutoka sehemu za mapaja na mabega.

‘Mchakato mzima wa mateso ya namna hii huendelea kwa karibu siku tatu ili kumlazimisha mteswaji kueleza au kukiri jambo na inakadiliwa kuwa mteswaji hukatwa karibu mikato 3,600 kabla ya kufariki dunia.’

Katika uchunguzi huo, pia tumebaini kuwa aina ya mateso ya kung’oa watu kucha pia yamekuwa yakitumiwa na watu wa Usalama wa Taifa nchini Iran, ambako wao hutumia mashine kumnyofoa kucha.

Wakati uchunguzi wa Mtanzania Jumapili ukibaini hayo, kumekuwa na hali ya hofu kwa jamii kuhusiana na matukio ya utekaji na utesaji kinyama yanayotekelezwa sasa kwa baadhi ya watu maarufu hapa nchini wanaotambulika kuwa na misimamo inayokinzana na ile ya serikali.

Tukio la kwanza lililoibua hofu ya kuwepo kwa kikundi maalumu chenye mafunzo ya kutesa na kuua ni lile la Dk. Ulimboka, ambaye akiwa katikati ya mzozo mkali na serikali kwa wadhfa aliokuwa nao wa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, alitekwa, akateswa vibaya na kwenda kutupwa katika msitu wa Pande, akiwa nusu maiti.

Dk. Ulimboka aliteswa kwa kupigwa mateke, ngumi, kung’olewa meno, kunyofolewa kucha na kuvunjwa baadhi mifupa ya mwili wake, zikiwemo mbavu. Mateso kama hayo ndiyo aliyoteswa nayo Kibanda.

RAIS KIKWETE AMJULIA HALI KIBANDA

Katika hatua nyingine, juzi Rais Jakaya Kikwete alimtembelea Kibanda katika hospitali aliyolazwa ya Mill Park, iliyopo mji wa Johannesburg, nchini Afrika Kusini kwa lengo la kumjulia hali.

Rais Kikwete alikuwa ameongozana na Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana.

Habari zinaeleza kuwa Rais Kikwete alitumia fursa ya kuhudhuria Mkutano wa Viongozi wa Vyama vilivyokuwa mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya ukoloni na ubaguzi wa rangi, unaofanyika nchini humo, kwenda kumuona Kibanda.

Taarifa zilizolifikia gazeti hili zinaeleza kuwa; Kikwete ambaye alizungumza na Kibanda kwa takribani dakika tano, alisema aliongea na Mwajiri wa Kibanda, ambaye alimueleza kuwa suala la matibabu alikuwa akilishughulikia, hivyo kwa upande wao serikali, itaendelea na uchunguzi na kuhakikisha wale wote waliohusika katika tukio hilo wanakamatwa.

KIBANDA AFANYIWA OPERESHENI

Madaktari bingwa watatu, wakiwemo wa kichwa na jicho, jana walimfanyia operesheni Kibanda, iliyochukua takribani masaa matano na nusu.

Katika operesheni hiyo ya kurekebisha taya na mishipa inayozunguka jicho, hata hivyo madaktari hao walishindwa kuokoa jicho lake na hivyo kuliondoa kwa ajili ya kumuwekea jingine la bandia.

Ripoti ya madaktari kuhusu kile kilichofanyika ndani ya chumba cha operesheni itatolewa leo.

Kibanda alivamiwa na watu wasiojulikana wakati anajiandaa kufunguliwa lango la kuingia nyumbani kwake, Mbezi Beach, jijini Dar es Salaam Machi 5 mwaka huu na kumjeruhi sehemu kadhaa za mwili wake na kisha kumng’oa meno, kucha na kumjeruhi vibaya jicho lake la kushoto.

Washirikishe Google Plus

About SeriaJr

SeriaJr will keep you updated with all current political news countrywide "Ndiye "Bosi" Mzito Arusha255" Karibu Tuhabarike!.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 maoni:

TANZANIA, THE HOME OF KILIMANJARO