Tunakusogezea karibu habari na matukio, zaidi habari za kisiasa na utawala, matukio ya Arusha na maeneo jirani, bila kusahau na mambo mengineyo ya kitaifa yanayojiri katika maeneo mbalimbali ya nchi kuhusu maendeleo na kuwa ya maslahi kwa watu wengi. Burudani na michezo pia havijasahaulika. Kizuri zaidi, unaweza kupata link ya Blogu nyingine na website muhimu hapa hapa kwa kuscroll mpaka chini. Karibu tuhabarike!

Mawaziri saba wang’oka, Mizengo Pinda chupuchupu

HATIMAYE mawaziri saba kati ya nane wakiwemo wanaokabiliwa na tuhuma za ubadhirifu, wamekubali kuandika barua za kujiuzulu wenyewe kwa kile kilichoelezwa kuwa ni kukinusuru Chama cha Mapinduzi (CCM).

Habari za kuaminika kutoka mjini Dodoma zimesema kuwa mawaziri hao, walilazimishwa kujiuzulu katika kikao cha dharura kilichokuwa chini ya uenyekiti wa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kilichofanyika mara tu baada ya kumalizika kwa kikao cha Bunge.

Taarifa zimewataja waliokubali kujiuzulu kuwa ni pamoja na Waziri wa Viwanda na Biashara, Cyril Chami; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Mkuchika; Waziri wa Uchukuzi Omari Nundu; na Waziri wa Afya, Dk. Haji Mponda.

Wengine wanaodaiwa kujiuzulu ni Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja; Naibu Waziri wa Afya, Lucy Nkya; na Naibu Waziri wa Viwanda, Lazaro Nyarandu.

Hata hivyo, Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo, ambaye alishambuliwa vikali kwa kuitwa kinara wa ufujaji, hakuwepo katika kikao hicho kwa madai kuwa yuko nje ya nchi, anasubiriwa aungane na wenzake kuachia ngazi.

Kujiuzulu kwa mawaziri hao kumekuja baada ya kuzuka kwa mjadala mzito ndani ya Bunge kwa siku mbili mfululizo kuhusiana na tuhuma za ufujaji wa kutisha wa fedha za umma, kiasi cha kusababisha kuwepo kwa azimio la kupiga kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu Mizengo Pinda.

Wakati wa majumuisho ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mashirika ya Umma, mwenyekiti wa kamati hiyo, Zitto Kabwe, alilitaka Bunge kuweka ushabiki na itikadi za kisiasa pembeni na kuazimia kwa pamoja kupiga kura za kutokuwa na imani na Pinda kutokana na uzembe wa mawaziri wake.

Kabla ya kujiuzulu huko Spika wa Bunge, Anne Makinda, jana alizima hoja ya kumwajibisha Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, akidai kuwa utaratibu mzima umekiukwa na hivyo hauwezi kufanyiwa kazi katika kikao cha sasa cha Bunge.

Makinda alisema hayo alipokuwa akitoa mwongozo uliyoombwa na Mbunge wa Bumbuli, January Makamba (CCM) kuhusu suala hilo na kudai kuwa wanaoendesha mchakato huo itabidi wasubiri hadi Bunge lijalo.

Makinda ametoa hoja hiyo, wakati idadi kubwa ya wabunge wakiwa wametia saini za kumwajibisha Waziri Mkuu kutokana na ubadhirifu mkubwa unaowahusisha mawaziri watano wa serikali.

Mchakato wa utiaji saini unaosimamiwa na Zitto Kabwe, ulikuwa ukiendelea kwa kasi na habari za kuaminika zinasema kuwa idadi ya walio tayari kuweka saini zao inaweza kufika wabunge 200.

Akuzungumza jana mchana, Zitto alisema kuwa hadi muda huo alikuwa na saini za wabunge 66, huku akidai kuwa wabunge wote wa CUF walikuwa wameandikiwa barua na chama chao kusaini azimio hilo, jambo ambalo litafanya idadi ya wabunge kufikia 80.

Zitto ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya kusimamia Mashirika ya Umma (POAC) alisema kuwa hadi jana majira ya saa 7 mchana, wabunge wa vyama vyote walikuwa wameweka saini azimio hilo isipokuwa wa UDP.

Mawaziri wanaotakiwa kuwajibika ni Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo; Waziri wa Viwanda na Biashara, Cyril Chami na naibu wake, Lazaro Nyalandu; Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Mkuchika; Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja; na Waziri wa Uchukuzi, Omar Nundu.

Zitto ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini (CHADEMA), alisema wabunge wa CUF 12 wameshasaini azimio hilo na kwamba maagizo yametoka makao makuu ya chama hicho kutaka wabunge wake kusaini kusudio hilo.

Alisema kuwa baadhi ya watu wanasema Waziri Mkuu hana makosa na kwamba anaonewa na kueleza kuwa wanampenda sana, lakini wanaiheshimu zaidi Tanzania.

Alisema kulingana na kanuni za Bunge, wabunge wanaweza kumwajibisha Waziri Mkuu kwa kumpigia kura ya kutokuwa na imani naye.

“Miongoni mwa majukumu ya Waziri Mkuu ni kusimamia shughuli za serikali pamoja na utendaji wa baraza la mawaziri. Mawaziri wameonekana kusimamia wizara zao ambazo zina wizi na ubadhirifu.

“Kuwepo kwa ubadhirifu ni kushindwa kwa Waziri Mkuu kutekeleza majukumu yake…tunajua hawezi kuwawajibisha mawaziri na ndiyo moja ya mambo tunayotakiwa kuyarekebisha kwenye Katiba, lakini yeye tuko naye hapa na sisi ndiyo tuliomthibitisha na tuna uwezo wa kuondoa uthibitisho wake.

“Kwa hiyo katika hilo hatuna mbadala hatuna muafaka kama mawaziri waliotajwa kuhusika na aina ya ubadhirifu kwenye wizara zao, idara zao, mashirika hayo na halmashauri kama hawajachukua hatua tunaanzia na Waziri Mkuu. Atakuwa Waziri Mkuu wa kwanza nchini kupigiwa kura au kutolewa hoja ya kutokuwa na imani naye.

“Tumempa muda mpaka Jumatatu tutawasilisha rasmi hoja yetu kwa Spika kwa mujibu wa mamlaka ya kanuni 133 inayotutaka kukusanya saini ya wabunge asilimia 20 ya wabunge wote ambao kwa hesabu zetu ni wabunge 70 na tutapata zaidi hao,” alisema.

Alisema kwamba wanatimiza matakwa hayo ya kikanuni na kisha kuwasilisha kwa Spika, ili baadaye Bunge liweze kuonyesha meno yake.

Alibainisha kuwa ili Waziri Mkuu aweze kutoka katika kitanzi hicho, anapaswa kumshauri Rais Jakaya Kikwete awafukuze kazi mawaziri hao ama mawaziri hao wajiondoe mapema.

“Lakini kama wanataka kumuweka kiongozi wao, kiraja wao rehani, wanataka Waziri Mkuu aingie katika hoja ya kupigiwa kura ya kutokuwa na imani naye ni jukumu lao, wachague wao wenyewe,” alisema.

Hata hivyo, Spika kwa upande wake alisema kwa mujibu wa kanuni za Bunge ambazo zimetokana na Katiba zinataka hoja kama hiyo iwasilishwe bungeni angalau siku 14 kabla ya siku iliyokusudiwa, na sio wiki ijayo kama ilivyoelezwa juzi na Zitto Kabwe bungeni.

“Sasa hii habari ya kusema waheshimiwa njooni njooni kusaini huo sio utaratibu. Hiyo haikubaliki kwa sababu mimi sijapata hiyo hoja mpaka sasa. Bunge hili tunaahirisha Aprili 23 maanake Jumatatu. Leo (jana), kesho (leo), Jumapili, Jumatatu haikidhi siku 14 sana sana anaweza (Zitto) kukusanya nyaraka labda kuwasilisha Bunge lijalo,” alisema Spika.

Aliendelea kusema kuwa kanuni na utaratibu alioutangaza Zitto hauwezekani na kwamba zoezi la kukusanya saini za wabunge ni batili. Aliwashauri wanaotaka hoja hiyo wavute subira hadi Bunge lijalo, akidai kuwa kuitimiza ndani ya siku tatu zilizobaki ni kukosa mashiko.

Hata hivyo alikiri kuwa wabunge wana madaraka na Waziri Mkuu kulingana na Katiba kwa kuwa ndiyo wanaomwidhinisha baada ya uteuzi.

Alinukuu ibara ya 53(a) (3) kwamba Waziri Mkuu anapitishwa na wabunge ambao wanamthibitisha. “Msingi wa Zitto ni kwamba huyu ni mtu tuliyempitisha sisi wenyewe. Kwa hiyo tuna mamlaka naye kwani ndiye tulimpitisha sisi,” alisema.

“Waziri ndiye atakayekuwa mkuu wa shughuli za serikali bungeni. Serikali chini ya mamlaka ya Rais ndiyo itakayofanya maamuzi juu ya sera. Na mawaziri chini ya uongozi wa Waziri Mkuu watawajibika kwa pamoja katika utekelezaji wa shughuli za serikali. Hivi vifungu ndivyo vinatupa nguvu ya kuwa na uwezo na Waziri MKuu.”

Wabunge wa CCM watishwa

Katika hatua nyingine, imedaiwa kuwa wabunge wa Chama cha Mapinduzi, wameitwa na kutishwa kuchukuliwa hatua ikiwa watasaini azimio hilo.

Mmoja wa wabunge wa CCM aliyekiri kuitwa ni Deo Filikunjombe (Ludewa) ambaye alisema alilazimika kusaini kabla ya kuitikia wito huo.

Filikunjombe, alikiri kuitwa na Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, na kumtaka kutosaini azimio hilo, lakini akamwambia alikwishasaini na alifanya hivyo kwa niaba ya wananchi wa Ludewa ambao wamechukizwa na ubadhirifu mkubwa uliofanywa na watendaji hao wa serikali.

Kuhusu wabunge wa CCM kutosaini azimo hilo, Filikunjombe alisema kanuni haikusema wabunge wote, kwani inafahamika wengine wanarudi nyuma alisema.

Mbunge wa Mtera Livingstone Lusinde alisema suala la hoja ya kikanuni ina lengo la kuchelewesha mchakato wa kuwaondoa wanaolalamikiwa na kuahidi kuwaondoa hata kama Bunge litawakingia kifua.

Alisema kama mawaziri wanaolalamikiwa wataendelea kubakia katika nafasi zao ni bora wabunge wa CCM wakaondoka na kuwaachia wao majukumu yote.

Alipoulizwa kama msimamo wake hauwezi kuwakera viongozi wake na kuamua kumchukulia hatua ikiwa ni pamoja na kumuondoa katika chama, Lusinde alisema kuwa hilo halihofii kwa kuwa hana hati miliki ya ubunge wa Mtera na zaidi ataendelea kubakia Mtanzania anayepigania maslahi ya nchi yake.

Mbunge wa Simanjiro, Christopher ole Sendeka (CCM), alisema katika mapendekezo yaliyoafikiwa juzi hakuna azimio katika kamati yoyote lililotaka waziri aondolewe na kusema kuwa alichokuwa akikifanya Zitto ni usanii.

“Katika taarifa yake ile alipaswa asema Bunge limependekeza mtu fulani awajibishwe, hivyo alitakiwa kuleta nyongeza katika taarifa yake. Hakuna aliyeleta. Ile ni burudani tu,” alisema na kuongeza kuwa hoja hiyo haina mashiko.

Alihoji kuwa iwapo Pinda alishindwa kumuondoa aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, David Jairo, atawezaje kumuondoa Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo.

Alisema kuwa ili hoja hiyo ifanikiwe ni lazima Spika aridhike kwamba ilifuata taratibu na ina sifa hata ikisainiwa na wabunge 200 kama haina sifa haiwezi kupita.

Zitto asema wembe ni uleule

Akizungumzia vikwazo hivyo, Zitto alisema haviwatishi na wanaendelea na mchakato huo, na kwamba watakabidhi hoja hiyo, Jumatatu baada ya kukamilika.

Zitto alisema kama watashindwa kusaini fomu hizo watakuwa wawakilishi wa ajabu kwa kuwa wao ndiyo waliokuwa wakipiga kelele juzi kutaka waliosababisha ubadhirifu kuwajibika na kwamba kama watashindwa kuunga mkono litakuwa ni jukumu la wananchi kupima uwakilishi wao.

Alisema ni jambo la aibu kwa Bunge zima likimaliza kikao bila kuwawajibisha mawaziri waliohujumu mali za taifa.

“Tukiondoka hapa bila kuwawajibisha watu, wananchi huko nje watalidharau Bunge kwa hiyo tunalinda heshima ya Bunge na kulinda heshima ya wabunge kwa kutaka kuona tunaimarisha uwajibikaji.

“Bila watu kuwajibika madudu haya yatarudia na ndiyo maana tunataka uwajibikaji ufanyike,” alisema.

Alisema kuwa anajua wabunge wa CCM wamechukizwa na wizi na ubadhirifu na wamesema kwa nguvu sana juzi na jana na hakuna asiyeona hilo.

“Mimi sijafanya kama mbunge wa CHADEMA, bali kama mbunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alisema.

Hivyo, alitaka wabunge wasigawanywe katika misingi ya vyama na kwamba anayefanya hivyo hana maslahi na nchi na kuhoji iwapo CCM ina hoja nzuri ambayo inaisimamia.

“Tusiruhusu maneno ya propaganda ya kutugawa na ninyi ndiyo mashahidi mnalalamika na juzi mlimuuliza CAG,” alisema.

Alisema katika masuala ya kitaifa wabunge wanapaswa kuweka pembeni itikadi zao na kuwatumikia wananchi wanaowawakilisha na kusisitiza kuwa wanachokitaka ni mabadiliko na si mapinduzi.

Wasomi waunga mkono

BAADHI ya wananchi wa kada na rika mbalimbali nchini wamesema mwenendo wa Bunge la sasa ni ishara za kuamka kwa mhimili huo inayotokana na changamoto za wabunge wa upinzani.

Wakizungumza na Tanzania Daima kwa nyakati tofauti wananchi hao walisema msimamo wa wenyeviti ambao ni wabunge kutoka upinzani wanaoongoza kamati tatu za Bunge umesaidia kuonyesha uozo wa watendaji serikalini hususan mawaziri wasiotimiza vema wajibu wao.

Wenyeviti wa kamati hizo ni Zitto Kabwe (CHADEMA) Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), Agustine Mrema (TLP) Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) na John Cheyo (UDP) Hesabu za Serikali (PAC).

Kwa mujibu wa Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) Profesa Issa Shivji, Katiba ya sasa inaruhusu kupiga kura ya kutokua na imani japo ni mapema kufanya hivyo huku akisisitiza kwamba jambo la msingi ni kusubiri uamuzi wa wabunge hao.

Kwa upande wake mhadhiri mwandamizi mstaafu wa UDSM Dk. Azaveli Lwaitama alisema wabunge hao wanagombana na mfumo wa kumweka Waziri Mkuu madarakani hali inayoonyesha wazi kwamba hawana imani na Rais.

“Ninavyoona hapo kinachowachukiza wabunge hao ni uwaziri mkuu na mfumo wa kumpata waziri mkuu kwa sababu wanalalamikia utendaji wa baadhi ya mawaziri lakini waziri mkuu hana uwezo wa kuwafukuza mawaziri hao.

“…Hebu tukumbuke wakati wa Jairo, Waziri Mkuu alitamani kumfukuza akashindwa lakini Katibu Mkuu Kiongozi alikuwa na uwezo; ndiyo maana alimpa likizo yenye malipo.

“Tatizo ni mfumo wa utawala walioteuliwa wanawajibika kwa aliyewateua lakini waliochaguliwa wanatumwa na wananchi ndiyo,” alisema Dk. Lwaitama na kuongeza kwamba lazima mambo hayo yaingie kwenye Katiba mpya.

Mjasiriamali Celina Ezekiel wa Isimani Iringa alisema Bunge limeanza kutambua mamlaka yake ya kuisimamia serikali hasa kwa wabunge wa CCM.

Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) Profesa Sifuni Mchome alisema wabunge wana uhuru wa kufanya hivyo kwa maslahi ya nchi na kuongeza kwamba ni jambo la kawaida.

Mkazi wa Igunga mkoani Tabora Nicholous Ngassa alisema haafikiani na suala la kumwondoa Waziri Mkuu madarakani badala yake mawaziri walioguswa na ripoti ya CAG wanapaswa kuwajibika na kupelekwa mahakamani.

“Hali ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu na serikali yake kunashusha thamani Chama cha Mapinduzi (CCM) katika jamii na kujiondoa kwenye ramani ya siasa nchini na Afrika,” alisema Ngassa.

Naye Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Idara ya Sayansi ya Siasa na Utawala Dk. Benson Bana alisema wabunge wametimiza wajibu wao na kuwataka mawaziri wanaotuhumiwa kuchukua hatua.

Akitolea mfano wa ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Dk. Bana ambaye ni mwenyekiti mwenza ya Taasisi ya Utafiti wa Elimu ya Demokrasia Tanzania (Redet) alisema umaskini unaongezeka kwa sababu ya wachache walio kwenye ngazi za uamuzi.

“Ripoti ya CAG inaonyesha kushuka kwa kiwango cha uwajibikaji serikalini hususan eneo la matumizi ya fedha za walipa kodi… kwa nini wanaotajwa kwenye ripoti hiyo wasijiuzulu?” alisema Dk. Bana na kutaka wabunge washikamane katika hilo.

Naye Mahadhiri wa Chuo Kikuu cha Kiislam cha Morogoro (MUM) Profesa Juma Mikidadi alisema wabunge wako sahihi katika uamuzi wa kutaka kumjadili Waziri Mkuu kwa sababu ya mawaziri wa chini yake kushindwa kuwajibika.

Sheikh Jabir Ramadhan aliwashauri wabunge hao kutoa muda wa mwisho kwa mawaziri hao ili kabla hawajaondoka waanze kuchunguzwa huku akiwashauri wasifanye hivyo kwa chuki.

Mkazi wa Tabata Jamila Athuman alisema serikali ya awamu ya nne imeongeza pengo kati ya matajiri wachache na maskini wengi hali inayowafanya wananchi kuichukia serikali yao.

“Walioteuliwa hawana uchungu wa nchi ndio maana wanafanya ufisadi huku Rais akiwakingia kifua kwa kuendelea kuwaacha madarakani na wakati mwingine anawahamisha vituo vya kazi,” alisema Jamila.

Joseph Mhimbilila alisema wananchi wamechoka kuvumilia wizi wa mali ya umma unaofanywa na watawala wao sasa wananchi wamechoka hivyo wabunge hao wakishindwa kuwasaidia watachukua hatua kali zaidi.

“Hili linaweza kuwa fundisho kwa viongozi wenye ndoto za kuliibia taifa hili,” alisema.

Kwa Upande wake Mwanasheria Alex Mgongolwa alisema sheria inampa mamlaka Waziri Mkuu kusimamia shughuli zote za serikali na kuhakikisha kunakuwepo na uwajibikaji.

Alisema katika Katiba ibara ya 53 (A 1-6) inasema hoja ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu inaweza kuwasilishwa bungeni kukiwa na sababu za msingi juu ya majukumu ya Waziri Mkuu na kushindwa kuyatekeleza.

“Nafuu inayoweza kupatikana ni kama anayetolewa hoja hajapitisha miezi sita tokea kuteuliwa kwake au kabla ya miezi tisa kupita tokea hoja kama hiyo kuwasilishwa bungeni, na hapa ni lazima Spika ajiridhishe kuwa masharti yamezingatiwa,” alisema Mgongolwa.

Chanzo: Tanzania Daima, 21 Aprili 2012

Washirikishe Google Plus

About SeriaJr

SeriaJr will keep you updated with all current political news countrywide "Ndiye "Bosi" Mzito Arusha255" Karibu Tuhabarike!.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 maoni:

TANZANIA, THE HOME OF KILIMANJARO