Tunakusogezea karibu habari na matukio, zaidi habari za kisiasa na utawala, matukio ya Arusha na maeneo jirani, bila kusahau na mambo mengineyo ya kitaifa yanayojiri katika maeneo mbalimbali ya nchi kuhusu maendeleo na kuwa ya maslahi kwa watu wengi. Burudani na michezo pia havijasahaulika. Kizuri zaidi, unaweza kupata link ya Blogu nyingine na website muhimu hapa hapa kwa kuscroll mpaka chini. Karibu tuhabarike!

Dk. Slaa: JK ameizika CCM kwa kuwapitisha watuhumiwa wa ufisadi kugombea

na Sitta Tumma, Mwanza (Tanzania Daima)

KATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibroad Slaa, amemvaa Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete, akisema amekitengenezea kaburi la kukizika rasmi chama chake kwa kuruhusu watuhumiwa wakubwa wa ufisadi kugombea nyadhifa mablimbali.

Dk. Slaa alisema uteuzi wa wagombea ndani ya CCM uliomalizika juzi umeonyesha wazi kwamba sasa chama hicho kinatumbukia kwenye dimbwi kubwa na pana lisiloweza kukitoa tena.

Akizungumza na Tanzania Daima jijini Mwanza, alikojichimbia kuhakikisha mchakato wa uchaguzi wa mameya wa jiji hilo unakwenda vizuri leo, Dk. Slaa alisema dhamira ya kweli dhidi ya CCM katika kuwaweka vijana kwenye uongozi ili kukinusuru chama hicho imezimika baada ya Kikwete kuruhusu watuhumiwa wa ufisadi na wakongwe kugombea uongozi.

“Katika hili la uteuzi wa CCM, nangojea taratibu zao zikamilike. Tulitegemea CCM muda huu ni wa kujisafisha, lakini imeshindwa kufanya hivyo. Mimi simung’unyi maneno kuhusu watuhumiwa wa ufisadi.

Mfano (anataja) ni fisadi wa fedha za rada. Mimi hapa nilishapeleka ushahidi hadi wa akaunti namba ya benki yake kwa DPP (Mkurugenzi wa Mashtaka Nchini), alisema.

Alisema inashangaza kuona katika utetezi wa CCM, mtuhumiwa huyo amepatiwa nafasi licha ya kushindwa kueleza wazi fedha nyingi kwenye akaunti hiyo ya Uswisi alizipataje.

“Mtuhumiwa mkubwa kama huyu wa ufisadi eti leo CCM inampitisha awe mgombea. Kweli? Sioni dhamira ya CCM kupambana na vitendo vya kifisadi. Na hata dhamira ya vijana haipo bali imejitumbukiza kwenye dimbwi ambalo kamwe hakitatoka humo,” alisisitiza.

Kuhusu Lowassa na tuhuma zake za ufisadi wa kampuni ya kufua umeme wa dharura wa Richmond zilizosababisha kujiuzulu uwaziri mkuu mwaka 2008, Dk. Slaa alisema kiongozi huyo alilazimika kujiuzulu kama sehemu ya kuwajibika, lakini ameshindwa hadi leo kumtaja mhusika hasa wa kampuni hiyo.

Alisema kama kweli Lowassa alisingiziwa katika tuhuma hizo, alipaswa kuwaeleza Watanzania nani anayehusika na ufisadi huo wa Richmond ambayo ilishindwa kuzalisha umeme licha ya kutumia mamilioni ya fedha za umma.

Kuhusu wanachama wa CCM ambao majina yao yamekatwa na NEC, Dk. Slaa alisema milango iko wazi CHADEMA kwa wale wasio mafisadi kujiunga ili kukielekeza chama hicho kushika dola mwaka 2015.

Alisema CHADEMA ni chama makini huenda kuliko vyama vingine, hivyo hakiwezi kupokea wanachama kutoka CCM wanaotuhumiwa kwa ufisadi, vinginevyo kitafunga milango na mapazia yake.

“Unajua, kuna watu wanaojulikana kwa ufisadi. Pia wapo wasafi wanaoomba kujiunga na CHADEMA, hivyo watu safi hawana tatizo kujiunga na CHADEMA kwa ajili ya kuunganisha nguvu kwenda kuongoza dola mwaka 2015,” alisema Dk. Slaa.

Mnyukano wa umeya

uchaguzi wa mameya wa wilaya mbili za Nyamagana na Ilemela jijini Mwanza, unatarajiwa kufanyika leo huku mnyukano mkali ukiwa katika halmashauri ya Nyamagana kutokana na CCM na CHADEMA kuwa na idadi sawa ya viti vya madiwani na hivyo kutegemea kura za CUF ziamue mshindi.

Katika Halmashauri ya Ilemela, CHADEMA ina uhakika wa asilimia mia moja kutokana na kuwa na madiwani wengi kuzidi wenzao wa CCM huku mikakati yao ikilenga kuwashirikisha CUF ili waitwae pia Nyamagana.

Uchaguzi huo unafanyika baada ya Halmashauri ya Jiji la Mwanza kugawanywa na hivyo kuzaa halmashauri hizo mbili. Lakini pia Halmashauri ya Jiji la Mwanza kwa sasa muda kadhaa haikuwa na Meya baada ya Baraza la Madiwani kumvua wadhifa huo, Jackson Manyerere (CHADEMA).

Baada ya meya kuenguliwa, kulizuka mtafaruku ndani ya CHADEMA jijini hapa ambao ulisababisha madiwani wawili kutimuliwa uanachama kwa kile kilichodaiwa ni usaliti wa kuanzisha hoja ya kumtosa kiongozi huyo.

Hivyo kutokana na CHADEMA kutokuwa na madiwani hao, inaingia kwenye uchaguzi wa leo ikiwa na madiwani sita na mbunge Ezekiel Wenje katika wilaya ya Nyamagana wakati wenzao CCM wana madiwani saba na CUF wawili.

Kwa mnyukano huo ni dhahiri kuwa CHADEMA na CCM watakuwa wamefungana kwa kura na hivyo kuhitaji huruma ya madiwani wa CUF ili upande mmoja uibuke kidedea.

Taarifa za uhakika kutoka jijini hapa ni kwamba CHADEMA wamefanya mazungumzo ya kushirikiana na CUF kwa kuwaachia nafasi ya Naibu Meya ambayo itagombewa na diwani wao wa kata ya Mirongo, Daud Mukama.

Kwa halmashauri ya Ilemela CHADEMA wana uhakika wa kuibuka kidedea kutokana na kuwa na madiwani wanane na mbunge Highness Kiwia huku wenzao wa CCM wakiwa na madiwani sita na CUF ina mbunge wa Viti Maalum, Mkiwa Kimwanga.

Kamati za utendaji za CHADEMA katika wilaya hizo zimefanya vikao tofauti kwa kushirikiana na kamati za madiwani na kukamilisha mchakato wa kupata wagombea wao.

Kwa mujibu wa ofisa habari wa CHADEMA, Tumaini Makene, kamati ya utendaji ya wilaya pamoja na madiwani wa Nyamagana walimteua aliyekuwa Naibu Meya kabla, Diwani wa Kata ya Maina, Charles Chibara, kuwa mgombea wa umeya wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza.

Kwa upande wa Ilemela, kikao cha kamati ya utendaji pamoja na madiwani walimteua Diwani wa Kata ya Nyamanoro, Abubakar Kapera, kuwa mgombea wa umeya Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela.

Kikao hicho cha Ilemela, pia kilimteua Diwani wa Kirumba, Danny Kahungu, kuwa mgombea wa nafasi ya Naibu Meya halmashauri hiyo wakati kamati ya utendaji ya Nyamagana imekubali kumwachia kugombea nafasi ya Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, Diwani wa Mirongo, Daudi Mkama (CUF).

Wao CCM wamemteua Diwani ya Kata ya Mkolani, Stanslaus Mabula, kugombea nafasi ya umeya katika halmashauri ya jiji la Mwanza huku diwani wa kata ya Igogo, John Minja, akigombea unaibu meya na Ilemela wagombea ni Renatus Kalunga na naibu wake Sarah Ng’hwanu.

Washirikishe Google Plus

About SeriaJr

SeriaJr will keep you updated with all current political news countrywide "Ndiye "Bosi" Mzito Arusha255" Karibu Tuhabarike!.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 maoni:

TANZANIA, THE HOME OF KILIMANJARO